Saturday, April 18, 2015

MSIKITI MORO WAWAKANA MAGAIDI


MSIKITI MORO WAWAKANA MAGAIDI
Kilombero. Wakati msikiti wa Sunni uliopo Kidatu wilayani Kilombero ukimkana Hamadi Makwendo aliiyeuawa katika tukio la kuwakamata watu 10 wanaotuhumiwa kuhusika na vitendo vya ugaidi, dereva wa bajaji iliyowabeba baadhi ya watuhumiwa hao, amemuelezea mtu huyo kuwa alikuwa hana shughuli za kikazi zaidi ya kucheza karate.

Polisi aliyejeruhiwa kwenye sakata hilo na ambaye amehamishiwa kwenye hospitali ya polisi mjini Morogoro, pia amesimulia mkasa uliosababisha ajeruhiwe huku kukiwa na taarifa kuwa watuhumiwa hao 10 wamehamishiwa jijini Dar es Salaam kwa mahojiano zaidi.
Watu hao walimakatwa mapema juzi usiku kwenye msikiti wa Sunni uliopo Kidatu baada ya wasamaria wema kulitaarifu Jeshi la Polisi kuhusu kuwapo kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu. 
Habari za uhakika zilizopatikana ndani ya Jeshi la Polisi zinasema watuhumiwa hao wamehamishiwa jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mahojiano zaidi.
Kamanda wa polisi wa mkoani hapa, Leonard Paul (pichani) hakupatikana kuzungumzia suala hilo na hata alipotafutwa kwa simu, mlinzi wake alipokea na kueleza kuwa bosi huyo wa polisi alikuwa kwenye kikao kuanzia asubuhi na hakujua angemaliza wakati gani.
Mmoja wa viongozi wa msikiti wa Masjid Salah Al – Fajih, Mohamed Manze alisema wao kama viongozi na waumini hawakuwa na taarifa zozote za ujio wa watuhumiwa hao, na kwamba katika msikiti huo wapo vijana wanne ambao huwa wanalala na kujisomea.
Alisema siku ya  tukio watuhumiwa hao walifika msikitini hapo saa 4:00 usiku wakati ibada ya mwisho ikiwa imeshafanyika na waumini kutawanyika.
Alisema walitumia mwanya huo kuingia na kujihifadhi bila taarifa zozote kwa uongozi wa msikiti huo, jambo ambalo ni kinyume na utaratibu za msikiti.
Hata hivyo, kiongozi huo alisema hawakupendezwa na suala hilo na kwamba limewachafua na kuwaharibia sifa waumini na msikiti wao. Alisema mtu aliyeuawa hakuwa muumini wa msikiti huo na hafahamiki.
Alisema hawana nasaba na kikundi chochote kinachojihusisha na uhalifu, na kulaani vikali watu wanaotumia dini hiyo katika masuala aliyoyaita kuwa ya kihalifu.
Dereva wa bajaji asimulia
Dereva  wa bajaji iliyobeba watuhumiwa hao katika kijiji cha Kidatu wilayani Kilombero, Alphonce Maulusi amemwelezea Hamad Makwendo, aliyeuawa kwenye tukio hilo kuwa  ni mtu aliyekuwa akijihusisha na mchezo wa kareti  pamoja na masuala ya dini na hakuwa na kazi maalumu
Mulusi alisema hayo jana wakati akiongea na waandishi wa habari waliotembelea kijijini hapo kwa lengo la kupata  undani wa tukio lililotokea juzi katika kijiji cha  Chikago kata ya Kidatu wilayani Kilombero ambapo watu 11 walikamatwa na polisi  msikitini wakiwa na vifaa mbalimbali vya milipuko pamoja na sare za jeshi.
Alisema siku ya tukio  majira ya saa 3:00 usiku akiwa katika eneo lake la kazi, walitokea watu 11 na kwamba watano kati yao pamoja na mwenyeji ambaye ni marehemu walipanda katika bajaji yake , na wengine sita walipanda katika bajaji ya mwenzake.
Alisema watu hao wakiongozwa na mwenyeji wao walitaka wapelekwe msikiti wa Sunni na kwamba wakati wote wa safari yao mwenyeji wao ndiye alikuwa akizungumza lugha ya Kiswahili huku wenzake wakisikiliza bila kujibu.
"Tuliwafikisha hadi eneo walilotaka na kisha tuligeuza na yule mwenyeji wao. Tulipofika Manyasini, tulisimamishwa na polisi waliotaka kujua tumetoka wapi na tunaenda wapi. Yule mwenyeji alishuka na kuanza kukimbia jambo lililofanya askari kuanza kumkimbiza huku sisi tukifuatilia nyuma," alisema.
Alisema mwenyeji huyo alipofika mbele kidogo alimkata polisi mmoja na jambia  na ndipo polisi walimpiga risasi na baadaye kumchukua na kumpandisha katika gari lao.
Alisema wananchi walifika katika eneo hilo na kuzingira gari hilo na kumshusha mtu huyo, huku wakitishia kuchoma moto gari la polisi . Akizungumzia  mwonekano wa watu hao, dereva huyo alisema walivalia mavazi ya jamii ya kabila la Wahindi maarufu kama Panjabi na umri wao ukionekana kati ya miaka 20 hadi 25 tofauti na mwenyeji wao aliyeonekana mkubwa wa zaidi ya miaka 30.
Koplo Nasoro Dabi, ambaye alijeruhiwa katika tukio hilo, alisema siku ya tukio, akiwa na askari wenzake walisimamisha bajaji iliokuwa na abiria mmoja,  Hamad Makwenda.
Alisema baada ya bajaji hiyo kusimama marehemu alikimbia hali, iliyoashiria kuwa ni mhalifu na hivyo kuwalazimu askari watatu, akiwamo yeye, kumkimbiza.
"Wakati tukimkimbiza, mimi nilikuwa mbele na tulipofika katika eneo lenye giza, alichomoa jambia na kuanza kunishambulia. Askari wenzangu waliokuwa nyuma yangu walifyatua risasi na kupiga nyingine juu hali iliyosababisha wananchi wengi kujitokeza na kuanza kumpiga kisha kumchoma moto," alisema.
Alisema wakati tukio hilo likiendelea askari wengine walifanya mawasiliano na mkuu wa  kituo cha Ruhembe na kuwaongezea nguvu.
Mwenyekiti wa kitongoji
Mweyekiti wa kitongoji cha Ikera, Mohamed Libaha alisema siku ya tukio hilo alifuatwa na askari saa 8:00 usiku na kutakiwa atoe malezo kama ana taarifa za wageni katika kitongoji chao.
Alisema bada ya kuwaambia kuwa hawana ugeni wowote, polisi waliwachukua watu hao pamoja na kiongozi wao wa dini, Ustadhi Maulid Sultani na kuondoka naye na hadi sasa hawana taarifa ya mintaarafu ya kiongozi huyo.
MWANANCHI