Thursday, April 02, 2015

CHE MPONDA AFARIKI DUNIA



CHE MPONDA AFARIKI DUNIA

MWASISI wa chama cha siasa, Tanzania People's Party (TPP), Dk Aleck Che-Mponda (80) amefariki dunia katika hospitali ya Massana iliyopo Mbezi Beach, Dar es Salaam alikokuwa amelazwa akisumbuliwa na maradhi ya saratani ya mifupa.



Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa mtoto wake, Chemi Che- Mponda, baba yake alifariki juzi jioni hospitalini hapo na kwamba mipango ya mazishi inafanywa nyumbani kwake Mbezi Beach.
Dk Che-Mponda alikuwa mwanasiasa na msomi wa sayansi ya siasa na aliwahi kuwa Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Idara wa Sayansi na Utawala mwaka 1980-1991.
Aidha, Dk Che Mponda alifanya utafiti muhimu kuhusu mgogoro wa mpaka kati ya Malawi na Tanzania kwenye Ziwa Nyasa mwaka 1971. Utafiti huo ulikuwa andiko la Shahada yake ya Udaktari wa Falsafa (PhD), katika Chuo Kikuu cha Howard, nchini Marekani.
Andiko hilo linaitwa, 'The Malawi- Tanzania Border and Territorial Disputes, 1968: A case study of Boundary and Territorial Imperatives in the new Africa'.
Akizungumzia kifo cha muasisi huyo msomi, Mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustine Mrema alisema kifo cha Dk Che-Mponda ni pigo kwa wanasiasa na wasomi nchini.
"Tumesikitishwa na kifo cha Dk Che- Mponda, alikuwa rafiki yetu, tulikua naye kwenye harakati za vyama vya siasa, alianza vizuri na ari kubwa na pia alikuwa msomi mzuri," alisema Mrema.
Aliongeza, kifo chake ni majonzi kwani ameondoka mtu muhimu aliyekuwa mcheshi na mwema kwa wanasiasa wengine na hata katika jamii

CHANZO HABARI LEO