Tuesday, April 19, 2016

SERIKALI YALAANI TUKIO LA KUNAJISIWA NA KUUAWA KWA MTOTO WA UMRI WA MIAKA TISA (9) MKAZI WA KIJIJI CHA KAPANGA, WILAYANI SUMBAWANGA



SERIKALI YALAANI TUKIO LA KUNAJISIWA NA KUUAWA KWA MTOTO WA UMRI WA MIAKA TISA (9) MKAZI WA KIJIJI CHA KAPANGA, WILAYANI SUMBAWANGA
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto inalaani vikali tukio La mauaji ya mtoto wa kike, umri miaka 9, ambaye alininajisiwa kwa zamu na watu wasiojulikana, na hatimaye kumkata mapanga yaliyosababisha kuuawa kwa mtoto huyo mdogo, katika kijiji cha Kapanga, wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa.

Wizara imepokea kwa huzuni kubwa taarifa kuhusu mazingira ya mauaji ya mtoto huyo, ambaye alifanyiwa ukatili mkubwa yaliyosababisha kifo cha mtoto huyo katika umri mdogo.

Wizara inapongeza agizo la Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, Paza Mwamlima, ambaye amelitaka jeshi la polisi wilayani Sumbawanga kuhakikisha wanawasaka na kuwatia mbaroni watuhumiwa wa mauaji ya mtoto ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya wahusika, na hivyo kuwa fundisho kwa watu wengine.

Wizara inapongeza ushirikiano uliooneshwa na wakazi wa kijiji cha Kapanga wilayani Sumbawanga, katika kumtafuta mtoto toka mafichoni kwa ajili ya kuokoa uhai wake. Jitihada zilizofanywa na jamii ya Kapanga ni uthibitisho kuwa, ulinzi wa mtoto ni jukumu la wazazi, walezi na watu wote katika jamii.

Kwa niaba ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee, na Watoto, tunatoa pole kwa marafiki wa mtoto, wazazi, ndugu na majirani na familia kwa ujumla, na tunawaomba kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki cha majonzi makubwa.

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
Erasto T. Ching'oro (Msemaji)
18/4/2016