Thursday, April 07, 2016

MAKAMPUNI YA NJE YASITISHWA KATIKA UANDAAJI WA MASTER PLAN NCHINI.


MAKAMPUNI YA NJE YASITISHWA KATIKA UANDAAJI WA MASTER PLAN NCHINI.

 Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; William Lukuvi (Mb), akitoa maagizo kadhaa wakati wa uzinduzi wa bodi mpya ya Wataalam wa Mipango Miji na Vijiji katika ukumbi wa Mikutano wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Kushoto kwake ni Mwenyekiti  mpya wa bodi hiyo; Prof. Wilbard Kombe na kulia kwake ni Mwenyekiti mstaafu, John Lubuva.

Mwenyekiti  mpya wa bodi ya Wataalam wa Mipango Miji na Vijiji; Prof. Wilbard Kombe akisisitiza jambo wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo katika ukumbi wa Mikutano wa  Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mwenyekiti mstaafu wa bodi ya Wataalam wa Mipango Miji; Bwn.John Lubuva akitoa taarifa fupi ya bodi hiyo, wakati wa uzinduzi wa bodi mpya katika ukumbi wa Mikutano wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. 

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi (Mb) ametangaza rasmi mwisho wa kutumia Makampuni ya nje katika kazi za kuandaa Master plan. Mhe. Lukuvi aliyasema hayo wakati akizindua rasmi bodi ya wataalam wa Mipango Miji Wizarani hapo.

Lukuvi amesema nchini kuna wataalam wengi na wenye elimu ya kutosha kwa ajili ya kufanya kazi ya kuandaa Master plan, lakini kumekuwa na taratibu za kutafuta wataalam hao kutoka nchi za nje. Alisema; " Ninaagiza kuwa sasa ni mwisho wa kuajiri makampuni ya nje, kazi za master plan zisimamiwe na bodi hii kwa kutumia makampuni ya humu humu nchini".

Ameendelea kusema kuwa' " Sasa Bodi ya Wataalam wa Mipango Miji itapaswa kuhusika kikamilifu katika zoezi la Upangaji, upimaji na umilikishwaji wa ardhi kwa kushirikiana na sekta binafsi na kuhakikisha kuwa suala la uwazi katika upangaji miji linazingatiwa".

Vile vile alisema kuwa bodi itapaswa kuhakikisha Wananchi wanashirikishwa kikamilifu katika kulipia gharama kadhaa kwa huduma wanazopatiwa na bodi. Mhe. Lukuvi alisema kuwa bodi hiyo haitaitwa tena bodi ya Mipango Miji, bali itajulikana kama bodi ya Mipango Miji na Vijiji.

Kwa upande wake Mwenyekiti mpya wa bodi; Prof. Wilbard Kombe alimuomba Lukuvi kuzitaka Halmashauri kushiriki vyema katika kutoa elimu kwa umma kwa kuwa na utayari wa kutoa taarifa zinazopaswa kuwasilishwa kwa Wananchi kwa wakati ili waweze kuelewa vyema kuhusu mipango inayohusu maeneo yao.