Saturday, August 01, 2015

Katibu CCM (W) akutwa na kura za maoni ofisini kwa mgombea



Katibu CCM (W) akutwa na kura za maoni ofisini kwa mgombea
Katibu wa CCM mkoa wa Mtwara, Shaibu Akwilombe

Chama cha Mapinduzi (CCM), mkoani hapa kimetengua uteuzi wa aliyekuwa katibu wa chama hicho wilaya ya Newala, Juma Namkoveka, baada ya kukutwa akichapisha kura za maoni kwenye ofisi ya mmoja wa watia nia ya ubunge.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake, Katibu wa CCM mkoa wa Mtwara, Shaibu Akwilombe, alisema katibu huyo alikutwa akichapisha karatasi hizo juzi saa 4 usiku katika ofisi ya Haroun Maarifa, ambaye ni Mkurugenzi wa kituo cha Radio Safari cha mjini Mtwara na mgombea ubunge wa jimbo la Newala mjini kupitia CCM.
 
Alisema kitendo cha karatasi hizo kukutwa katika ofisi ya mgombea ubunge hakiwezi kuaminiwa na wagombea wengine wanaowania jimbo hilo na hakistahili kufanywa na mgombea yeyote ili kuepusha migongano ya kimasilahi baina yao.
 
Alisema baada ya kukamata karatasi hizo zilipelekwa katika vyombo vya ulinzi na usalama kwa ajili ya kuzihifadhi, na kwamba jana alizichukua na kuzipeleka wilayani Newala ambako ndiko eneo sahihi lililotakiwa kuchapisha na sio mjini Mtwara kama ilivyofanywa na katibu huyo.
 
"Katika mazingira kama hayo kwa wagombea wengine wanaweza wakapata mashaka...Sasa baada ya kuchukua hizi hatua za mwanzo za kuhakikisha kwamba karatasi zinakuwa salama, tumeamua kwamba zikitoka polisi zile karatasi nitakabidhiwa na nitakwenda nazo Newala," alisema.
 
"Nikifika Newala nimemteua kaimu katibu wa wilaya mwingine, anaitwa Jenifer Chingwile, ni katibu msaidizi na muhasibu wa wilaya ya Tandahimba na nimeagiza nimkute Newala..lakini wakati huo huo aliyekuwa katibu wa wilaya ya Newala nimetengua mamlaka yake ya kiuchaguzi kuanzia leo na nimekwishampa barua yake..."
 
Alisema katibu huyo alikosa umakini kwa kile alichokifanya, na kwamba kwa mtu makini hawezi kuchukua karatasi za kupigia kura na kuzipeleka nyumbani au ofisini kwa mgombea kwa namna yoyote, kwani kila wilaya inapaswa kutengeneza karatasi hizo kwa gharama zake.
 
Aidha, alisema waligundua kuwa karatasi za jimbo la Newala vijijini ambako Maarifa  anakogombea zilikuwa zimepungua kutoka  karatsi 26,000 hadi 21,000.
 
Katibu aliyesimamishwa, Juma Namkoveka, alipotakiwa kuzungumzia suala hilo alikanusha na kukataa kuzungumza chochote.
NIPASHE ilimtafuta Maarifa ambaye ni katibu mwenezi wa CCM mkoa, na kukana kutambua taarifa hizo.