Friday, April 10, 2015

Kitindamimba familia ya Rais Kikwete ataka ubunge B’moyo


Kitindamimba familia ya Rais Kikwete ataka ubunge B'moyo

Rais Jakaya Kikwete 
Makada wawili wa CCM wilayani Bagamoyo,  wameonyesha nia ya kuingia kwenye kinyang'anyiro cha ubunge katika jimbo hilo kupambana na mbunge wa sasa, Dk Shukuru Kawambwa.
Makada hao ni Mwenyekiti wa CCM kata ya Dunda, Yusufu Mrisho Kikwete ambaye ni kitinda mimba wa familia ya Rais Jakaya Kikwete na Abdursharrif Zahoro ambaye  ni mwenyekiti wa Jumuia ya Wazazi  CCM wilayani humo.
Wakati  makada hao wakitangaza nia hiyo  juzi, tayari  mbunge wa jimbo hilo Dk Shukuru Kawambwa  alikwisha tangaza nia ya kutaka kutetea nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Tambo za wapinzani wa Kawambwa
Abdulsharrif alisema ameamua kuingia katika kinyanganyiro hicho baada ya  makundi mbalimbali ya wakazi wa wilaya hiyo, wakiwemo  kina mama na vijana kumuomba achukue fomu ili aweze kuwania nafasi hiyo.
 "Nimefuatwa sana jamani na wananchi wa hapa, wakati mwingine hadi naona aibu kujificha maana nahisi ni Mungu amewaonyesha kiongozi anayewafaa safari ijao, kwa hiyo nimekubaliana na maombi hayo, nitajitokeza kukabiliana na Dk Kawambwa," alisema.
Naye Yusuph Kikwete alisema  ana matumaini makubwa ya kushinda kwa kuwa, amekuwa akiungwa mkono na makundi mbalimbali, wakiwamo vijana ambao wamekuwa wakimshawishi kugombea nafasi hiyo.
 "Ni kweli kuna makundi mengi, yamekuwa yakinishawishi kuingia katika kinyang'anyiro na baada ya kutafakari sana na kujipima kama ilivyo kwa wanasiasa wengine, nimeona siwezi kukataa ushawishi huo, maana kuna watu wameona uwezo wangu  wa kiuongozi," alisema.
Mapema wiki hii  Dk Kawambwa aliweka wazi kuwa anaingia tena katika kinyang'anyiro hicho kutokana na kuridhishwa na mambo mbalimbali aliyofanya kwa wapigakura wa jimbo hilo.
 "Ninarudi  na wana Bagamoyo wameniomba nifanye hivyo  kutokana na kufanya mengi ya maendeleo, mfano katika kipindi changu cha miaka kumi, nimeweza kushughulikia changamoto kubwa zilizokuwa zikiwakabili wakazi wa jimbo hili, ikiwamo masuala ya elimu, afya na maji.
"Lakini kubwa, ni kushughulikia matatizo ya ardhi na malipo ya fidia," alisema.