Tuesday, March 13, 2012

MARTHA MWAIPAJA APIGWA NDOA








Na Gladness Mallya
BAADA ya maombi ya muda mrefu hatimaye mwimbaji wa nyimbo za Injili, Martha Mwaipaja ametimiza ahadi yake ya pili ulimwenguni baada ya Machi 4, mwaka huu kufunga ndoa (kupigwa ndoa) na Mchungaji John Said, Ijumaa linakudokeza.
Martha na mumewe walifunga ndoa hiyo katika Kanisa la Udhihirisho la Gongo la Mboto jijini Dar ambalo linamilikiwa na mumewe huyo na kuhudhuriwa na watu wengi wakiwemo waimbaji wengine wa nyimbo za Injili.
Mara baada ya kufanikisha tendo hilo takatifu, Martha alimshukuru Mungu kwa kupata mume kwa kuwa hilo ndilo lilikuwa ombi lake la muda mrefu.
“Nawasihi wenzangu ambao hawajaolewa kufanya maombi kwa muda mrefu bila ya kukata tamaa, naamini kuwa Mungu atawasikia kama alivyoyasikia maombi yangu na kuwapa waume wa kuwafaa,” alisema.
Katika hali iliyowafurahisha waliohudhuria ndoa hiyo, Martha aliimba wimbo maalum kwa ajili ya ndoa yake na kuserebuka sebene la Yesu pamoja na mumewe huku wakisaidiwa na waumini wengine.
Ndoa hiyo ilifuatiwa na sherehe ya nguvu iliyofanyika katika Ukumbi wa Delax, Sinza jijini ambapo watu walikula, wakanywa na kusaza huku wakiburudika na nyimbo za Injili.

Kwa hisani ya GLOBALPUBLISHERS