Friday, April 10, 2015

ALIYEKUTWA NA BASTOLA KANISANI AACHIWA


ALIYEKUTWA NA BASTOLA KANISANI AACHIWA
Mkazi wa Kijitonyama, Dar es Salaam, Joseph Mumbi ambaye alikamatwa na polisi Kisarawe akishukiwa kutaka kufanya uhalifu wa kutumia bastola siku ya Ibada ya Ijumaa Kuu ilipokuwa ikiendelea katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Stephano, ameachiwa jana kwa dhamana.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ulrich Matei alisema Mumbi ameachiwa baada ya Polisi kujiridhisha na maelezo ya awali aliyoyatoa pamoja na kuwasilisha  vielelezo vilivyothibitisho uhalali wa umiliki wa silaha hiyo .
Hata hivyo, Kamanda Matei alisema pamoja na kupata dhamana, polisi bado wanaendelea na uchunguzi ili kujiridhisha kama hakuwa na nia mbaya.
Alisema madai kuwa alikuwa hatulii wakati wa misa pamoja na kitendo chake cha kushika simu yake ya kiganjani mara kwa mara kama mtu aliyekuwa akitaka kufanya mawasiliano kiasi cha kuwafanya waumini wamshuku kuwa alitaka kufanya uhalifu, ndiyo yanayowafanya waendelee kumchunguza.
Kamanda Matei aliongeza kuwa, tayari simu ya mkononi aliyokua akiitumia kwa mawasiliano siku hiyo imepelekwa Ofisi ya Kampuni ya Tigo ili wafuatilie mawasiliano yaliyofanyika siku hiyo.
"Tigo wanafuatilia mawasiliano ya simu hiyo halafu watatutaarifu ili nasisi tukamilishe uchunguzi wetu kuhusiana na jambo hili," alisema Kamanda Matei.
Mumbi alishukiwa kuwa huenda akawa ni mhalifu kutokana na muonekano wake uliotia shaka.