Thursday, July 03, 2014

JK aomboleza kifo cha Nkwabi Ng’wanakilala


JK aomboleza kifo cha Nkwabi Ng'wanakilala
Nkwabi-Ng'wanakilala
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametuma salamu za rambirambi kuomboleza kifo cha mwandishi wa habari mkongwe na mhadhiri mwandamizi katika Chuo Kikuu cha Mt. Augustine, Bwana Nkwabi Ng'wanakilala.
Bwana Ng'wanakilala ambaye alifariki dunia mwishoni mwa wiki kwenye Hospitali ya Rufani ya Bugando mjini Mwanza kwa matatizo ya figo na tumbo, alizikwa  Jumatatu, Julai Mosi, 2014, nyumbani kwake Kibamba, Dar es Salaam.
Katika salamu ambazo amemtumia Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mt. Augustine, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais Kikwete amesema: "Kifo hiki kimelinyang'anya taifa letu mmoja wa wanataaluma wa habari mahiri sana na mtumishi hodari wa umma ambaye alithibitisha sifa hizo katika nafasi zote alizozishikilia. Tasnia ya habari imepoteza kiongozi hodari."
Ameongeza Rais Kikwete: "Alithibitisha sifa hizo kwenye nafasi ya Ukurugenzi wa Idara ya Habari, kwenye Ukurugenzi wa Redio Tanzania Dar Es Salaam (RTD) na kwenye Ukurugenzi wa Shirika la Habari Tanzania (SHIHATA). 

Aidha, marehemu alithibitisha vipaji vyake siyo kwenye uandishi wa habari tu bali hata kwenye uandishi wa vitabu, utafiti na uhadhiri, shughuli ambayo ameifanya hadi mauti yalipomfika."
"Naungana na wanafamilia, wanajumuia ya Chuo Kikuu cha Mt. Augustine na wanataaluma wa tasnia yote ya habari nchini kuomboleza kifo cha Bwana Ng'wanakilala. Aidha, naungana nao katika kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke pema roho ya Marehemu Nkwabi Ng'wanakilala. Amina."