Sunday, May 25, 2014

MBWA MWITU’ WAITEKA MITAA DAR


MBWA MWITU' WAITEKA MITAA DAR
kamanda                    72872
Polisi jijini Dar es Salaam wamelazimika kutumia mabomu kulitawanya kundi la vijana zaidi ya 300 wanaojiita 'Mbwa Mwitu' lililokuwa limewavamia wananchi na kupora mali kwenye nyumba na maduka.
Wakizungumza na gazeti hili, wakazi wa Mtaa wa Kigogo Mkwajuni, wilayani Kinondoni ambapo vurugu hizo zilitokea, walisema kuwa vijana kadhaa walifika mtaani hapo juzi Alhamisi saa 9:00 alasiri na kudai kuwa walipewa kibali cha kupiga muziki wa mnanda katika Barabara ya Mwembejando.
Muda mfupi baada ya kuanza kuimba na kucheza muziki, kundi hilo lilifunga barabara ya mtaa huo, huku vijana wengine kutoka sehemu mbalimbali za wilaya hiyo wakizidi kuelekea katika eneo hilo.

"Kwa mara ya kwanza jana (juzi) niliona watu wanne wamepakizana kwenye bodaboda, wote walikuwa wanafuata mnanda. Sijui huo muziki una nini ukipigwa unakusanya sana watu," alisema Mjumbe wa Serikali ya Mtaa, Ramadhan Liganduka.
Akizungumza kwenye ofisi ya Serikali ya Mtaa, mjumbe huyo alisema kuwa alishtushwa na kundi la vijana lililokuwa likiingia mtaani kwake kwenda kwenye muziki wa mnanda ambao umepigwa marufuku, ndipo alipompigia simu Ofisa Mtendaji wa mtaa huo, Magreth Mpinge.
"Nilimpigia simu nikwamwambia ninasikia mnanda unapigwa, hali siyo salama huko. Niliwapigia simu hata majirani na wapangaji wangu nikawaambia hali siyo nzuri wasijiamini sana, huo muziki huwa unaambatana na fujo," alisema.
Alisema baada ya kupigiwa simu, Polisi walifika katika eneo hilo saa 2:15 usiku wakati huo tayari vijana hao walikuwa wameshaanza kupora mali kwenye maduka na kwa wapita njia.
Mmoja wa wakazi walioshuhudia tukio hilo, Humphrey Massawe alisema kuwa wakati muziki ukiendelea baadhi ya vijana walikuwa wakitumia nafasi hiyo kupora simu za watu waliokuwa wanakwenda kucheza muziki, jambo lililowalazimisha watu kuanza kufunga maduka kwa hofu.
"Jana (juzi) hapa ilikuwa kama Sudan, watu walituvamia wengi kama 300 hivi, sura zao ni ngeni walikuwa wanapora mali kwenye maduka.
"Mimi niliambiwa na mwenzangu kuwa watu wanavamia maduka huko chini, kwa hiyo nifunge duka langu, lakini niliogopa kutoka nje nifunge kwa sababu milango inafungwa kwa nje," alisema Massawe.
Aliongeza kuwa polisi walipofika katika eneo hilo walichukua vyombo vyote vya muziki na kuondoka navyo, pia waliwakamata baadhi ya wakazi mtaani hapo. Mtendaji wa mtaa huo, Magreth alisema kuwa hakuna mwenyeji aliyejeruhiwa, lakini kijana mmoja anayedhaniwa kuwa ni mmoja wa vijana hao alipigwa na kuumizwa wakati wa purukushani hizo.
"Ni mapema mno kujua jina la huyo kijana na sehemu alikotoka, ndiyo kwanza tunaendelea kufuatilia. Wale huwa hawaendi hospitali, waende huko wakakamatwe?" alihoji.
Magreth alisema kuwa watu kadhaa wanashikiliwa na Polisi wakiwamo waliotoa umeme utumike kupiga muziki, ambao haukuwa na kibali.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso, alisema vimeibuka vikundi mbalimbali vya vijana jijini Dar es Salaam vinavyojulikana kama Mbwa Mwitu, Watoto wa Mbwa au Panya Road, ambavyo vimekuwa vikijihusisha na uporaji, unyang'anyi wa kutumia nguvu na kujeruhi watu.
Senso alisema, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Abdulrahman Kaniki amewaagiza makamanda hususan wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kuhakikisha wanavitafuta vikundi hivyo popote vilipo, kuwakamata na kuwafisha katika vyombo vya sheria.
"Naibu IGP amekemea vikali vikundi hivyo na kuvitaka kuacha tabia hiyo mara moja, kwani vitendo hivyo ni vya kihalifu na vinatakiwa kukemewa na kila mtu katika jamii.
"Aidha, amewataka wananchi kuondoa hofu na badala yake watoe ushirikiano kwa kutoa taarifa za vikundi hivyo katika vituo vya Polisi ili zichukuliwe hatua za haraka," alisema.
CHANZO MWANANCHI