Sunday, November 18, 2012

RAGE AMTIMUA ZITTO KABWE SIMBA


 
Mbunge wa Chadema Zitto Kabwe 

KUBORONGA kwa Simba Ligi Kuu Bara kumekoroga mambo ndani ya klabu hiyo. 

Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage amevunja kamati zilizokuwa zinaundwa na waziri na wabunge kadhaa. Rage pia amelifuta tawi maarufu la Mpira Pesa la Magomeni jijini Dar es Salaam. 

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana Ijumaa kwenye Makao Makuu ya Simba, Rage alidai amechukua hatua hiyo ili kurudisha utulivu klabuni na kuongeza ufanisi. 

Fagio hilo limewakumba Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Amosi Makala, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, Mbunge wa Kilwa-Kusini (CCM), Murtaza Mangungu na Mbunge wa Kilombero (CCM), Abdul Mtekete, aliyewahi kuichezea Simba na Pan African. 

Vigogo hao walikuwa wajumbe wa Kamati ya Fedha na Uchumi iliyokuwa chini ya Makamu Mwenyekiti, Geofrey Nyange 'Kaburu'. 

Kamati nyingine zilizovunjwa ni ya usajili, ambayo bosi wake alikuwa Zacharia Hans Pope, Kamati ya Mashindano chini ya Joseph Kitang'are 'Mzee Kinesi', Ufundi iliyokuwa inaongozwa na Ibrahim Masoud 'Maestro' na ya Nidhamu iliyokuwa chini ya Peter Swai. 

Rage alisema wanachama wa Mpira Pesa, wamekuwa wakihusika kupitisha karatasi la saini za wanachama ili kuitisha mkutano bila idhini ya Kamati ya Utendaji kinyume cha katiba ya Simba. 

Alikwenda mbali zaidi na kutangaza kuwang'oa Mwenyekiti wa tawi hilo, Masoud Awadhi na anayejiita Mwenyekiti wa Wanachama, Ally Bani kwa kukiuka katiba ya Simba. 

Wanachama hao walishiriki kutembeza karatasi lililofikisha saini zaidi ya 700 na walikuwa na uwezo wa kuitisha mkutano wa wanachama ili kuupindua uongozi. 

Rage alisema katika uchunguzi wao pia wamegundua watu zaidi ya 80, si wanachama hai na wengi walikuwa wanatumia stakabadhi feki kulipia ada ya uanachama. 

"Tumewaruhusu kuunda tawi jingine kama watajikusanya tena," alisema Rage. 

Hata hivyo, Awadh alijibu mapigo kwa kudai kuwa wao walifuata katiba kwa kuomba saini za wanachama waliofika 700 kama katiba inavyotaka na ameahidi kupeleka suala lao kwa Msajili wa Vyama na Klabu za Michezo wa Wilaya ya Ilala.