Friday, April 27, 2012

Hukumu ya TUNDU LISSU LEO!



 Na Elisante John
Singida,

 
KESI inayomkabili mbunge wa Singida mashariki kwa tiketi ya CHADEMA, Tundu Lissu, iliyofunguliwa mjini Singida kupinga ushindi uliomweka madarakani, itatolewa leo ijumaa (Aprili 27, mwaka huu).
 
Hukumu itatolewa na Jaji Moses Mzuna, anayesikiliza kesi hiyo, iliyofunguliwa na makada wawili wa CCM, Shabani Itambu na Pascal Hallu.
Kesi hiyo imekuwa kivutio sana kwa wananchi wengi wa mkoa Singida na nchini kwa ujumla, kutokana na umaarufu wa mbunge huyo machachari.
Jaji anayesikilia shauri hilo mjini Singida, anatoka mahakama kuu kanda ya Kilimanjaro.
Walalamikaji wa kesi hiyo, iliyofunguliwa mahakama kuu kanda ya Ddoma, wanatetewa na wakili Godfrey Wasonga, kutoka mkoani Dodoma, na Lissu amejisimamia mwenyewe.
Kesi hiyo ilianza kusikilizwa Machi 12, 2012, kufuatia makada wawili wa CCM, kupinga ushindi wa Lissu kwa madai kuwa uchaguzi huo uligubikwa na dosari nyingi.
Katika mahojiano na Lissu, amesema vyovyote mahakama itakavyo hukumu, anajivunia kuimarisha demokrasia na kuwa mbunge wa kwanza kutoka upinzani, kwenye historia ya mikoa ya kanda ya kati.
Amesema, kanda hiyo ilijulikana sana kuwa ngome ya CCM, lakini amefanikiwa kuchaguliwa na wananchi ili awatumikie.