Wednesday, April 20, 2016

SERIKALI YAPIGA MARUFUKU MIFUKO YA PLASTIKI



SERIKALI YAPIGA MARUFUKU MIFUKO YA PLASTIKI
Waziri wa Nchi, Ofisi ya                Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba

SERIKALI imepiga marufuku uzalishaji na matumizi ya mifuko ya plastiki, kuanzia Januari Mosi mwakani.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba alipiga marufuku jana bungeni wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Njombe Mjini, Edward Mwalongo (CCM).

Mwalongo alitaka kujua lini Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira itakaa na wadau wa mazingira kujadili suala la uzalishaji na matumizi ya mifuko hiyo ambayo imekuwa ikiongoza kwa uchafuzi wa mazingira.

January alisema sasa wanaendelea kufanya majadiliano kuhusu suala hilo na kwamba Januari Mosi mwakani itakuwa mwisho wa uzalishaji na matumizi ya mifuko ya plastiki nchini.

Awali, akijibu swali hilo la nyongeza, Naibu Waziri katika ofisi hiyo, Luhaga Mpina alisema Serikali itawachukulia hatua za kisheria wenye viwanda vya kuzalisha mifuko ya plastiki ambao wanakiuka sheria na taratibu zilizowekwa.

"Wadau wote, wazalishaji na viwanda wanatakiwa kuhakikisha wanazalisha mifuko inayoruhusiwa yenye unene usiopungua mikroni 50, tutachukua hatua kwa viwanda vitakavyokiuka ikiwemo kufunga viwanda hivyo," alisema Mpina.

Alisema elimu itaendelea kutolewa ili kuwakinga wananchi na madhara yanayotokana na matumizi ya mifuko hiyo.


HABARI LEO