Monday, February 22, 2016

WAZIRI MHAGAMA ALITAKA BARAZA LA UWEZESHAJI (NEEC) KUTEKELEZA PROGRAMU ZAKE KWA WAKATI



WAZIRI MHAGAMA ALITAKA BARAZA LA UWEZESHAJI (NEEC) KUTEKELEZA PROGRAMU ZAKE KWA WAKATI
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge, Sera, Kazi, Ajira ,Vijana na Walemavu, Bi.Jenista Mhagama kushoto akikaribishwa na Katibu Mtendaji wa Bazara Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), Bi.Beng'i Issa, wakati alipofanya ziara ya kwanza ya kukutana na watumishi wa sekretarieti ya Baraza la hilo.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge, Sera, Kazi, Ajira Vijana na Walemavu, Bi.Jenista Mhagama kulia akizungumza na watumishi wa sekretarieti ya Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) hawapo pichani, mara baada ya kufanya ziara yake ya kwanza ya kujifunza kazi za baraza hilo, kushoto Katibu Mtendaji wa Bazara hilo, Bi.Beng'i Issa.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge, Sera, Kazi, Ajira ,Vijana na Walemavu, Bi.Jenista Mhagama akizungumza na watumishi wa sekretarieti ya Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), mara baada ya kufanya ziara yake ya kwanza ya kujifunza kazi za baraza hilo mwishoni mwa wiki, kushoto Katibu Mtendaji wa Bazara hilo, Bi.Beng'i Issa.


Serikali imelitika Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) kuhakikisha linayafikia malengo iliyojiwekea ya uwezeshaji wananchi kiuchumi ili kupunguza tatizo la ajira kwa vijana hapa nchini.
"Kama baraza mna jukumu la kufanya kazi kwa bidii na vitendo ili kuwawezesha wananchi kiuchumi na kupunguza tatizo la ajira," Waziri Mhagama alitoa wito huo mwishoni mwa wiki alipoitembelea sekretarieti baraza hilo jijini Dar es Salaam. 
Alisema Serikali ya Awamu ya Tano inapenda kuona kazi zinafanyika kwa vitendo na matokeo yake yanawanufaisha wananchi na siyo vinginevyo. 
Alisema baraza ni chombo kikubwa cha kitaifa na kimepewa dhamana kubwa ya kuwawezesha wananchi kumiliki uchumi wao na kuondoa tatiazo la ajira kwa vijana , hivyo wanawajibu wa kutekeleza majukumu yao kwa vitendo.
"Tukiweza kuwawezesha watanzania kiujuzi, mitaji na vitendea kazi kulingana na makundi yao kwa kushirikiana na wadau wetu, tutakuwa tumewatendea haki watanzania na sisi tutakuwa katika nafasi nzuri",alisema Bi. Mhagama.
Alisema makundi hayo ya vijana wanajishughulisha na kilimo, ufugaji, ujenzi, vijana wa vyuo vikuu, Vijana wahitimu wa mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na vija wote wakiwemo badaboda na biashara mbalimbali.
"Tukiwafikia hawa wote  taifa hili badala ya kutembea litakuwa linakimbia na kufikia uchumi wa kati ifikapo 2025,"alisema.
Waziri Mhagana alilitaka baraza hilo kujiwekea muda wa utekelezaji wa programu zake ili kwenda na wakati sababu serikali inataka kila programu ianze kwa muda mwafaka na kwisha kwa muda mwaka.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Bazara hilo, Bi. Beng'i Issa alisema baraza limejipanga kutekeleza maagizo ya waziri na mipango yake kwa ufanisi na kwa muda uliopangwa kuhakikisha azma ya kuwawezesha watanzania kiuchumi inafikia malengo.

"Baraza hadi sasa linatekeleza mkakati wa kitaifa wa uwezeshaji ambao tayari umeshasambazwa kwa watekelezaji" na pia kunamwongozo wa kitaifa wa mafunzo ya ujasiriamali ambao upo mbioni kuanza kufundishwa kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu, aliongeza kusema.Bi Issa. 
Aidha alisema baraza pia linatekeleza mwongozo wa makakati wa kitaifa wa uwezeshaji wananchi Kiuchumi (NMSFEE), madawati ya uwezeshaji yameanzishwa katika ngazi ya kitaifa,mikoa, halmashauri na sekta mbalimbali kufuatilia taarifa za uwezeshaji.

Pia alisema programu ya majaribio ya  kijana jiajiri imenaza kutekelezwa kwa kutoa mafunzo, malezi na mitaji kwa vijana wa miaka 18 hadi 35 kwa mikoa ya Mtwara, Lindi, Dar es Salaam na Morogoro na unalenga kusambazwa nchi nzima.
Suala la watanzania katika kushiriki katika uwekezaji unaofanyika nchini kutoka nje (local content) katika sekta zote unashughulikiwa kwa kushirikiana na wizara zinazohusika na masuala haya ili watanzania wasiweze kuachwa nje ya uchumi wao.
"Sekta zilizopewa kipaumbele katika jambo hilo ni pamoja na madini,mafuta na gesi asilia, ujenzi, biashara ya maduka, Kilimo na viwanda na biashara,"alisema Katibu Mtendaji huyo.

Naye Mkurugenzi wa Mfuko wa Uwezeshaji (Empowerment Fund),Bw. Edwin Crisant alisema kuanzia mwaka 2007 hadi 2015 baraza limetumia Tsh. bilioni 2.5 kudhamini mikopo iliyotolewa na Benki ya CRDB yenye thamani ya Tsh. bilioni 10.47 kwa wajasirimali 10,769 na vikundi 300.
Pia baraza limeingia mikataba zaidi na benki na taasisi mbalimbali zikiwemo za Benki ya Posta, NSSF, Jeshi la Kujenga Taifa na Benki ya maendeleo ya Kilimo kutoa mafunzo kwa vijana na kudhamini mikopo yao kwa ajili ya shughuli za kiuchumi.