Friday, December 04, 2015

DUKA LA DAWA MUHIMBILI LAZINDULIWA



DUKA LA DAWA MUHIMBILI LAZINDULIWA

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Donan Mmbando amezindua duka la dawa la Bohari Kuu ya Dawa (MSD) lililofunguliwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kutekeleza agizo la Rais John Magufuli.

Uzinduzi wa duka hilo ulifanyika siku chache baada ya Dk Magufuli kuiagiza MSD kufungua duka hilo ili kurahisisha huduma kwa wananchi wanaofuta dawa nje ya hospitali hiyo. Akizindua duka hilo, Dk Mmbando alisema Serikali haina mpango wa kufunga maduka yaliyopo nje ya hospitali hiyo kwa sababu yana vibali pia yamefuata sheria na taratibu za nchi zinazotakiwa.
"Serikali haina mpango wa kufunga maduka yaliyopo nje ya hospitali ya Muhimbili bali itaimarisha huduma zake kwa kuuza dawa kwa bei nafuu ili kuleta unafuu kwa wagonjwa," alisema Dk Mmbando na kuagiza duka hilo liwe na dawa za kutosha ili kukidhi mahitaji.
Alisema kwa kufanya hivyo, maduka mengine yanayouza dawa kwa bei ya juu yatajiondoa yenyewe. Alisema MSD haitaishia katika duka hilo, bali itakwenda katika hospitali nyingine za rufaa, mikoa na wilaya.

CHANZO:Habari leo