Thursday, December 10, 2015

BALOZI SEIF ALI IDDI AMEMUAGIZA MKURUGENZI WA ‘ZAWA’ KUFANYA UCHUNGUZI WA KINA NA KUWACHUKULIA HATUA ZA NIDHAMU KWA MUJIBU WA SHERIA WATENDAJI WA MAMLAKA HIYO.



BALOZI SEIF ALI IDDI AMEMUAGIZA MKURUGENZI WA 'ZAWA' KUFANYA UCHUNGUZI WA KINA NA KUWACHUKULIA HATUA ZA NIDHAMU KWA MUJIBU WA SHERIA WATENDAJI WA MAMLAKA HIYO.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiwasili mtaa wa Mlandege kukagua kiwanja cha nyumba ya Ghorofa kinacholalamikiwa na Wakaazi wa Mtaa huo kwamba kimevamia pia eneo la wazi linalotumika kwa shughuli za Kijamii.
Mmiliki wa Kiwanja cha nyumba ya Ghorofa Mlandege Bwana Anuari Abdullah akijitetea kupata kibali kinachomruhusu kuendeleza ujenzi wa nyumba yake.

 Baadhi ya Wakaazi wa Mtaa wa Mlandege wakitafakari na kufurahia maamuzi yaliyochukuliwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif ya kuzuia ujenzi wa jengo la Ghorofa kwa kukosa taratibu zinazozingatia Mji mkongwe wa Zanzibar.

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amemuagiza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar { ZAWA } kufanya uchunguzi wa kina na kuwachukulia hatua za nidhamu kwa mujibu wa sheria watendaji wa Mamlaka hiyo wanaotumia dhamana yao katika kusimamia huduma za maji kwa njia ya kuwanyanyasa Wananchi.

Alisema zipo dalili za wazi zinazoonyesha kwamba baadhi ya Watendaji wa Mamlaka hiyo wanatekeleza majukumu yao ya kazi kwa kuendesha utashi wao binafsi zaidi wa kisiasa.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa agizo hilo wakati akiwapa pole Wananchi wa Shehia ya Dole Wilaya ya Magharibi "B" mara baada ya kukagua mifereji ya huduma za Maji safi na Salama ya wananchi wa Shehia hiyo ambayo ilikatwa na mengine kung'olewa kabisa vianzio vyake kufuatia operesheni iliyofanywa na watendaji wa Mamlaka hiyo.

Opereshi hiyo ya Tarehe 22 Oktoba iliyoathiri nyumba 24 zenye familia 22 ililalamikiwa na Wananchi hao kwa vile ilitekelezwa siku mbili tu kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Tarehe 25 Mwezi Oktoba mwaka huu ikionyesha wazi kuwa baadhi ya watendaji wa Mamlaka hiyo waliweka utashi wao wa Kisiasa.

Balozi Seif alisema Tabia iliyofanywa na baadhi ya Watendaji hao wa Zawa ya kuendesha operesheni hiyo kwa kumsingizia yeye ndie aliyeagiza kutekelezwa ilikuwa na lengo la kumchafua kisiasa.

Alisema hilo ni jambo linaloonekana kupangwa maalum ndani ya kipindi cha kuelekea kwenye uchaguzi Mkuu ambalo si vyema likachanganywa pamoja kati ya huduma za Kijamii na itikadi za Kisiasa.

Akiwapa pole Wananchi hao wa Dole kwa kukosa huduma za maji safi aliwataka watendaji wa Mamlaka ya Maji kuhakikisha kwamba huduma hiyo katika Shehia ya Dole inarejeshwa tena kama kawaida ndani ya kipindi cha wiki mbili zijazo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maji Zanzibar { ZAWA } Dr. Mustafa Garu aliahidi kutekeleza agizo hilo na kuwaeleza Wananchi hao kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inachokifanya kwao ni kuwataka wachangie huduma za Maji safi na salama ili kuiwezesha Mamlaka hiyo ipate nguvu zaidi za kuimarisha miundo mbinu yake.

Alisema takwimu ziko wazi zikionyesha kwamba Serikali Kuu imekuwa ikibeba gharama za upatikanaji wa huduma za Maji safi na salama kwa zaidi ya asilimia 65% wakati punguzo lililobaki la asilimia 35% tu huomba kuchangiwa na Wananchi.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amemuagiza Mmiliki wa Kiwanja kinachotaka kujengwa Nyumba ya Ghorofa katika Mtaa wa Mlandege Bwana Anuari Abdulla kusitisha mara moja ujenzi huo.

Hatua hiyo ya Balozi Seif imekuja kufuatia malalamiko makubwa yaliyotolewa na wakaazi wa Mtaa huo wakimshutumu Mmiliki huyo kuvamia pia eneo la wazi { Open Space } la shughuli za kijamii katika sehemu hiyo.

Balozi Seif alimuonya Mmiliki huyo kwamba endapo ataendelea kukaidi agizo alilopewa na Mamlaka Nne zinazosimamia na kushughulikia masuala ya Ujenzi Serikali italazimika kumchulia hatua za kisheria dhidi yake.

Alifahamisha kwamba wakaazi wa Mtaa wa Mlandege ambao wanaishi ndani ya eneo la Mji Mkongwe lililopata hadhi ya kuwa Urithi wa Kimataifa wanapaswa kuzingatia matakwa yaliyokubalika katika uhifadhi wa Mji huo wa Kihistoria.

Mapema Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uhifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe wa Zanzibar Nd. Issa Sarboko Makarani alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Mmiliki wa kiwanja hicho amekuwa akikaidi maamuzi anayopewa kuyatekeleza na mamlaka husika katika ujenzi huo.

Nd. Sarboko alisema Bwana Anuari ameamua kuendeleza ujenzi huo kwa kutumia kibali alichopewa na Mmoja wa Afisa wa Baraza la Manispaa ambacho tayari kimeshafutwa kwa vile kinakiuka na kutozingatia sheria na taratibu zilizowekwa.

Alisisitiza kwamba Mmiliki huyo tayari ameshaonywa na Viongozi wa Taasisi Nne waliokutana kujadili suala hilo na kumtaka asubiri maamuzi ya pamoja yatakayotolewa baada ya kuzingatia hali halisi ya namna yatakavyozingatia matakwa na haki ya kila upande unaohusika.

Alimtaka Mmiliki huyo kuhakikisha kwamba mabati yaliyowekwa kufunga eneo la wazi lililokuwa likitumika kwa wapita njia pamoja na kutumika kwa shughuli za Kijamii anayaondoa mara moja vyenginevyo watendaji wa Mamlaka hiyo watalazimika kutekeleza amri hiyo kwa kutumia kijiko katika kipindi kifupi kijacho.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

10/12/2015.