Wednesday, August 26, 2015

Lawrence Masha apelekwa Segera hadi taratibu za dhamana kukamilishwa


Lawrence Masha apelekwa Segera hadi taratibu za dhamana kukamilishwa

Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha leo amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu jijini Dar es Salaam na kusomewa shitaka la kutoa lugha ya matusi kwa maofisa wa polisi hapo jana.

Baada ya kusomewa shitaka hilo, Masha amekana na kurudishwa Segerea hadi hapo nyaraka zake zilizowasilishwa kwa ajili ya dhamana zitakapohakikiwa.

Masha amefikishwa mahakamani hapo akiwa na vijana wengine 19 ambao wamesomewa shitaka la kutaka kukusanyika bila kibali.

Awali taarifa zinasema Masha alifika katika Kituo cha Polisi cha Osterbay jijini Dar es Salaam jana jioni kwa lengo la kutaka kuwadhamini vijana hao na baadaye alishikiliwa na polisi kituoni hapo.

Masha alikihama Chama cha Mapinduzi hivi karibuni na kujiunga na Chadema na kuteuliwa kugombea Ubunge katika Jimbo la Sengerema katika Uchaguzi Mkuu wa mwezi Oktoba.