Tuesday, January 27, 2015

Wahitimu JKT kuandamana tena kwenda Ikulu



Wahitimu JKT kuandamana tena kwenda Ikulu
Rais Jakaya Kikwete.

Wahitimu wa mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kuanzia mwaka 2000 hadi 2014,  wanatarajia kuandamana tena keshokutwa kwenda Ikulu jijini Dar es Salaam kuwasilisha kilio chao cha kukosa ajira kwa muda mrefu. 

 
Vijana hao wameamua kuandamana kwenda kuwasilisha kilio chao hicho kwa Rais Jakaya Kikwete baada ya  kuandika barua tatu kwenda Ikulu  bila  kujibiwa. 
 
Akizungumza kwenye mkutano wa vijana hao Mwenyekiti wa Umoja huo,  George Mgoba,  alisema vijana wengi wamekuwa wakipelekwa kwenye mafunzo ya JKT  na kuahidiwa kupatiwa ajira na serikali huku wakiishia mitaani.
 
"Jumatano  tutaandamana kwenda Ikulu kumuona Rais na kumfikishia kilio chetu cha kukosa ajira kwa miaka yote hiyo kwani tunaamini wanaomwakilisha wanamdanganya kwa kudai kuwa vijana wote waliomaliza JKT wameajiliwa sehemu mbalimbali kitendo ambacho siyo,"alisema Mgoba
 
Alihoji sababu za serikali kuwapeleka vijana kwenye mafunzo hayo wakati haina uwezo wa kuwaajiri.
 
Mgoba alisema chakushangaza JKT hiyo hiyo inaajiri  vijana  wanaotoka visiwani Zanzibar  lakini wanaotoka Bara wanarudishwa nyumbani.
 
Alisema hata ajira ambazo zimekuwa zikitolewa ni kwa upendeleo na kwa vijana wasio na sifa kitendo ambacho hakiwatendei haki.
 
 Vijana hao waliandamana Desemba17,  mwaka jana kwenda Ikulu kuonana na Rais Kikwete lakini  Jeshi  la Polisi  Kanda Maalumu jijini Dar es Salaam liliwazuia na  kuwataka kuteua viongozi watano wa kuwasilisha malalamiko yao.
 
Hata hivyo, hawakufanikiwa kuonana na Rais Kikwete na baadala ya kukutana na wasaidizi wake.