Friday, January 23, 2015

Kinana apiga MARUFUKU ziara za mikoani za Mwigulu Nchemba kwa madai kuwa zina harufu mbaya ya Kampeni za Urais



Kinana apiga MARUFUKU ziara za mikoani za Mwigulu Nchemba kwa madai kuwa zina harufu mbaya ya Kampeni za Urais
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM (Tanzania Bara), Mwigulu Nchemba amekubali kuitikia wito wa kusitisha ziara zake za kichama katika mikoa na wilaya mbalimbali nchini, kama alivyoagizwa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana.
Katika barua yake ya Januari 18, mwaka huu, Kinana alimwagiza Mwigulu ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mbunge wa Jimbo la Iramba Magharibi mkoani Singida, kusitisha mara moja ziara zote na kwamba endapo atataka kufanya hivyo, atalazimika kutoa taarifa na kupata kibali.
Akizungumza jana na Paparazi, Mwigulu alikiri kupokea barua hiyo, na kusema hana tatizo na kusitisha ziara zake za kichama, kwani ni maagizo halali ya mamlaka ya juu yake kichama.
"Haya ni maelekezo, na siku zote kwa kuwa nafanya kazi kwa mujibu wa Katiba, sioni tatizo kupokea maelekezo rasmi ya kiofisi…aliyeniagiza ni kiongozi wangu katika chama, nitafanya hivyo," alisema kiongozi huyo kijana, lakini machachari katika ulingo wa siasa.
Katika siku za hivi karibuni, amekuwa akipasua anga kwa kutumia helikopta katika ziara zake alizofanya mikoa ya Tanga na Morogoro.
Mwigulu alisema amekuwa akipokea mialiko mingi ya kichama, hivyo anajikuta akitumia muda wake wa ziada wa siku za mwishoni mwa wiki kufanya ziara, lengo likiwa kutenganisha muda wa utendaji wake katika chama na serikalini.
"Ndiyo maana nilikuwa nafanya ziara za kichama siku za mwisho wa wiki pekee…na baada ya Morogoro pia nimealikwa Kigoma, Mafia (Pwani), Kagera, mikoa ya Kusini na Njombe. Kwa ujumla mialiko ni mingi, lakini nitaifanya kwa kufuata maelekezo. 
  
"Sitavunja sheria za chama wala za nchi hata siku moja, nitawatumikia wananchi kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa," alisisitiza Mwigulu.
Barua hiyo ambayo Kinana alimwandikia Mwigulu tarehe 18 Januari mwaka huu, mwaka huu ilisomeka hivi: 
"Umekuwa ukifanya ziara nyingi katika mikoa na wilaya bila ushirikishwaji kamili wa Makao Makuu, Mikoa na hasa Kamati za Siasa. Wewe pia umeonesha kwa kauli na mienendo yako kujiandaa kugombea nafasi ya Urais kupitia CCM. Ziara hizi zina mwelekeo wa kampeni, jambo ambalo ni kinyume na maadili ya Chama. Nakuagiza kuzisitisha ziara zote. Iwapo utataka kufanya ziara yoyote ya Kichama itabidi kwanza uniarifu na upate kibali changu. Nakuagiza utekeleze agizo hili mara moja".
Hata hivyo, mara zote alizoulizwa kuhusu kuwania Urais mwaka huu, Mwigulu amekuwa haweki wazi dhamira hiyo kama inavyoelekezwa.
  
Lakini, amekuwa akisisitiza amekuwa akiombwa kufanya hivyo na makundi ya watu mbalimbali, wakiwemo wanasiasa, wasomi, wakulima na wafanyakazi, vijana, wazee, wanawake na wanaume