Wednesday, January 14, 2015

BREAKING NYUZZZZ...: TAKUKURU YAANZA KUWABURUZA WASHTAKIWA WA ESCROW MAHAKAMANI


BREAKING NYUZZZZ...: TAKUKURU YAANZA KUWABURUZA WASHTAKIWA WA ESCROW MAHAKAMANI
Watu  wawili Rugonzibwa Mujunangoma na Theophillo Bwakea wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, wakikabiliwa na mashitaka ya rushwa baada ya kupokea mgao wa Sh. Milioni 485.1 kutoka kwenye akaunti ya Tegeta Escrow walizohamishiwa na James Rugemalira.

Katika kesi ya kwanza, aliyekuwa Mwanasheria wa Mamlaka ya Vizazi na Vifo (Rita) Mujunangoma ambaye kwa sasa ni Mkurugenzi wa Sheria Wizara Ardhi, Nyumba Maendeleo ya Makazi, alisomewa mashitaka yake mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Emmilius Mchauru.

Upande wa Jamhuri ukiongozwa na Mwendesha Mashitaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai akisaidiana na Max Ari, ulidaiwa kuwa Februari 5, mwaka 2014 katika benki ya Mkombozi iliyopo Ilala jijini, mshtakiwa akiwa Mkuu wa Sheria wa wizara hiyo, alipokea rushwa.

Ilidaiwa kuwa mshtakiwa alipokea rushwa ya Sh. Milioni 323.4 kama zawadi kupitia akaunti yake namba 00120102062001 kutoka kwa Mshauri binafsi wa kimataifa na Mkurugenzi wa zamani wa IPTL,James Rugemalira baada ya kuwa mjumbe katika menejimenti ya Rita wakati wa machakato wa kuipitisha IPTL kuiuzia Tanesco umeme.

Ilidaiwa kuwa mshtakiwa alipokea zawadi hiyo kama ofisa wa muda wa kushughulikia masuala ya IPTL. Mshtakiwa alikana mashitaka yake.

Swai alidai kuwa upande wa Jamhuri hauna pingamizi la dhamana na kwamba mahakama ijielekeze katika hati ya mashitaka fedha anazodaiwa kuchota mshtakiwa.

Hakimu Mchauru alisema mshtakiwa atakuwa nje kwa dhamana kwa kujidhamini kwa Sh. Milioni 160 taslimu au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo ya fedha.

Pia wadhamini wawili wanaofanyakazi serikalini watakaosaini hati ya dhamana ya Sh. Milioni 10 na mshtakiwa asitoke nje ya Dar es Salaam, bila kibali cha mahakama.

Mshtakiwa alitimiza baadh ya masharti ya dhamana ambapo hakimu alisema mahakama imempa dhamana ya muda hadi Januari 16, mwaka huu hati za mali zake zitakapohakikiwa.

Katika kesi ya pili, aliyekuwa mjumbe wa kitengo cha kuidhinisha Tanesco kununua umeme wa IPTL, Wizara ya Nishati na Madini, Injinia Bwakea kwa sasa mtumishi wa Wakala wa Umeme Vijijini(REA), alisomewa mashitaka yake mbele ya Hakimu Mkazi Frank Moshi.

Swai alidai kuwa Februari 12, mwaka 2014 mshtakiwa akiwa Injia Mkuu wa REA, alipokea rushwa ya Sh. Milioni 161.7 kupitia akaunti namba 00410102643901 ya Tegeta Escrow kama zawadi kutoka kwa Mkurugenzi Rugemalira.

Ilidaiwa kuwa mshtakiwa alipokea zawadi hiyo baada ya kuwa mjumbe aliyeandaa sera zinazohusu sekta binafsi kuzalisha na kuuza umeme kwa Tanesco.

Mshtakiwa alikana mashitaka yake. Upande wa Jamhuri ulidai kuwa hauna pingamizi la dhamana na kwamba upelelezi umekamilika.

Hakimu Moshi alimtaka mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili kutoka serikalini au wanaofanyakazi katika taasisi zinazotambulika watakaosaini hati ya dhamana ya Sh. Milioni 20 kila mmoja. Pia alisema mshtakiwa asitoke nje ya Dar es Salaam,  bila kibali cha mahakama.

Mshtakiwa alitimiza masharti ya dhamana na kesi yake itatajwa Januari 26, mwaka huu. 

Leo kuanzia  saa 2:00 asubuhi katika viunga vya mahakama ya Kisutu, watumishi na watu mbalimbali waliingia katika eneo hilo huku kukiwa na minong'ono kwamba wanaotuhumiwa ufisadi wa Escrow watafikishwa mahakamani hapo.

Pia waandishi wa habari waligawanyika katika makundi tofauti huku wakijadili na kutafatuta wadau wao kujua kuhusu ujio wa watuhumiwa hao.
Mapema jana saa 5:42 asubuhi vigogo hao walitinga mahakamani hapo na kwenda kusomewa mashitaka yao yanayowakabili.