Friday, January 30, 2015

Akutwa amekufa, mwili wake watundikwa mtini



Akutwa amekufa, mwili wake watundikwa mtini WATU wawili wameuawa katika matukio tofauti, akiwemo kijana mmoja ambaye hajafahamika jina wala makazi yake.

Kijana huyo alikutwa amenyongwa na watu wasiofahamika kisha mwili wake kutundikwa juu ya mti kwa kutumia suruali aliyokuwa amevaa katika kijiji cha Ibadakuli, Manispaa ya Shinyanga.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Longinus Tibishubwamu alisema tukio hilo limetokea Januari 27, mwaka huu. Alisema mwili ulikutwa na jeraha kwenye mguu wa kulia na uchunguzi wa daktari unaonesha kuwa kijana huyo aliumia kabla ya kunyongwa shingo na chanzo cha mauaji hayo hakijajulikana.

Wakati huo huo, Kamanda Tibishubwamu alisema mwanamke asiyefahamika jina wala makazi yake anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 25 na 30 ameuawa kisha mwili wake kuwekwa chini ya daraja dogo lililopo katika kitongoji cha Jihingu kata ya Kolandoto manispaa ya Shinyanga.

Aliongeza kuwa mwili wa marehemu umekutwa ukiwa na majeraha kichwani, usoni na ubavuni na kwamba Jeshi la Polisi linafanya uchunguzi juu ya mauaji hayo ili kuwabaini na kuwakamata wahusika.