Sunday, October 12, 2014

GABRIEL FUIME AFUTIWA KESI YA MAUAJI NA KUWA MAUAJI BILA KUKUSUDIA


GABRIEL FUIME AFUTIWA KESI YA MAUAJI NA KUWA MAUAJI BILA KUKUSUDIA
 Aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Gabriel Fuime akifikishwa mahakamani wakati wa hatua za awali za kesi hiyo.
 ------------------------
Na Mwene Said wa Globu ya Jamii
 MAHAKAMA Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, imefuta  mwenendo wa kesi ya mauaji iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini dhidi aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Gabriel Fuime na wenzake 11, wanaohusishwa na kuporomoka kwa jingo la ghorofa 16 katika mtaa wa Indira Gandh na kuua watu 27 badala yake wafunguliwe mashitaka ya kuua bila kukusudia.
 
Akisoma uamuzi huo,Jaji Salvatory Bongole Ijumaa iliyopita baada ya kukubaliana na hoja zilizowasilishwa mbele yake na mawakili wa upande wa utetezi kuwa na mashiko ya kisheria. Jaji Bongole aliamuru washtakiwa kuendea kushitakiwa kwa makosa ya zamani ya kuua bila kukusudia na siyo makosa ya mauaji.
 
Alisema washtakiwa wanastahili kuendelea kuwa nje kwa dhamana zao kama livyokuwa kabla upande wa Jamhuri kubadilisha hati ya mashitaka yao Marchi 12, mwaka huu kutoka mauaji ya bila kukusudia na kuwa kesi ya mauaji ya kukusudia.
 
 Jengo lililoporomoka Marchi 29, mwaka 2013 katika mtaa wa Indira Gandhi ulioko katika wilaya ya Ilala, jijijini Dar es salaam na kuua watu 27. 
Jaji alitupilia hoja za upande wa Jamhuri ulikuwa ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Bernard Kongola kuwa hati ya mashitaka ya mauaji ya kukusudia iliyowasilishwa mahakamani ilikuwa sahihi na inajitosheleza kuwawezesha washitakiwa kupanga utetezi wao. Katika uamuzi wake uliopokelewa kwa shangwe na washitakiwa na ndugu zao waliokuwa wamefurika katika viunga vya  Mahakama Kuu, Jaji Bongole alisema kuwa kitendo cha kubadilisha mashitaka kutoka mauaji ya bila kukusudia hadi mauaji ya kukusudia kulifanywa kwa nia mbaya na upande wa Jamhuri.
 
Alieleza kuwa upande wa mashitaka ulikuwa na nia ya kuwafanya washtakiwa wabaki rumande na hii ilidhihilishwa tangu awali pale walipofikishwa kwa mara ya kwanza kwa kosa la mauaji ya bila kukusudia na upande wa mashitaka ukapinga dhamana.
 
Mara baada ya Mahakama ya Kisutu kuwapa washtakiwa dhamana upande wa Jamhuri ulikata rufaa kupinga dhamana hiyo. Hata hivyo, Jaji Bongole alifafanua kuwa upande wa Jamhuri uliachana na rufaa hiyo mara baada ya mwaka mmoja kupita uliwasilisha Mahakama ya Kisutu maombi ya kubadilisha hati ya mashitaka ya mauaji ya kukusudia.
 
"Mabadiliko haya hayakufanywa kwa nia njema bali yalilenga kuwanyima haki washtakiwa… Vitendo vya makusudi vya namna hii havikubaliki na vinapaswa kukoma mara moja," alisisitiza jaji huyo wakati akisoma uamuzi wa kuwabadilishia washtakiwa hao hati ya mashitaka.
 
Mbali na Fuime, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Razah Ladha (68), Goodluck Mbaga (35), Wilboard Mugyabuso (42), Mohamed Abdulkari (61), Charles Ogare (48), Zonazea Oushoudada (60), Vedasto Richale (59), Michael Hemed (59), Albert Munuo (56), Joseph Ringo (43) na Ibrahim Mohamed.
 
Katika kesi ya msingi, upande wa Jamhuri unadai kuwa Marchi 29, mwaka 2013 katika mtaa wa Indira Gandhi ulioko katika wilaya ya Ilala, washtakiwa hao waliwaua watu 27. 
Katika tukio hilo watu 27 walipoteza maisha wakiwemo Yusuph Khari, Kulwa Alfan, Hamada Musa, Kessy Manjapa, Hamis Mkomwa, Boniface Bernard, Suhail Karim, Salman Akbar, Selemani Haji, Selemani Mtego, Sikudhani Mohamed, Ahmed Milambo na Salum Mapunda.
 
Wengine ni Selemani Mnyamani, John Majewa, Mussa Mnyamani, Devid Herman, William Joakim, Abdulrahaman Mwiha, Emmanuel Christian, Mmanyi Ngadula, Adivai Desiki, Emmanuel Wahai, Augustino Chuma, Gabriel Godwin Kamwela, Philipo Kusimula, Betod Mwananengule na Zahda Abbas