Sekretarieti ya CPA Kanda ya Afrika                  inasikitika kutangaza kifo cha aliyekuwa Katibu Mkuu wa                  Jumuiya ya Madola, (CPA) Dkt. William Ferdinand Shija                  (pichani) kilichotokea katika Hospitali ya Charring                  Cross, London Uingereza tarehe 4 Oktoba, 2014.
        Taarifa ya kifo chake imekuja wakati                  ambapo Mkutano wa 60 wa CPA unafanyika Yaoundé,                  Cameroon. 
        Dkt. William Shija amefanya kazi kwa                  takriban miaka 8 kama Katibu Mkuu wa Chama cha Wabunge                  wa Jumuiya ya Madola. Amefanya kazi kubwa kwa CPA na                  ameacha rekodi kubwa ya utendaji wa kazi akiwa pia ndio                  Katibu Mkuu wa kwanza kutoka Afrika katika Chama hicho.                  
        Katika uhai wake, Dkt. William Shija                  amefanya kazi ikiwa ni pamoja na kushikilia nyadhifa                  zifuatazo katika Serikali ya Tanzania:-
        §  Waziri wa                  Viwanda na Biashara;
        §  Waziri wa                  Nishati na Madini;
        §  Waziri wa Habari                  na Utangazaji 
        §  Waziri wa                  Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu; na 
        §  Mkuu wa Mkoa wa                  Mwanza.
        Aidha, Dkt. William Shija amekuwa Mbunge                  kwa takriban miaka 15. Akiwa Mbunge, Dkt. William Shija                  alikuwa Mwenyekiti na Mjumbe katika Kamati zifuatazo:- 
        §  Mambo ya Nje; na
        §  Habari;                  Utamaduni na Utalii.
        Vile vile, amewahi kuwa Mbunge wa Bunge                  la Afrika ambapo aliongoza Timu ya Uangalizi wa Uchaguzi                  kutoka Bunge hilo kwa Uchaguzi Mkuu wa Malawi mwaka                  2004.
        Kitaaluma, Dkt. Shija amesoma na kuhitimu                  Shahada za Uzamili na Uzamivu katika Chuo Kikuu cha                  Howard Nchini Marekani. Alisoma na kuhitimu Shahada ya                  kwanza na Stashahada ya Uandishi katika Chuo Kikuu cha                  New Delhi. Amefanya kazi kama Mhadhiri Mwandamizi katika                  Chuo cha Maendeleo ya Jamii, Nyegezi na pia amewahi                  kufundisha katika Chuo cha Utumishi wa Umma na Chuo cha                  Uhazili Tabora.
        Dkt. Shija ameacha Mke Bibi Getruda Peter                  Shija na watoto watano; Leo, Anna, George, Ferdinand na                  Monica.
        Sekretarieti ya CPA kwa kushirikiana na                  Familia ya marehemu, Bunge la Tanzania, Ubalozi wa                  Tanzania nchini Uingereza na Mwajiri wake CPA Makao                  Makuu na CPA Makao Makuu inaratibu mazishi yake ambapo                  mwili wa marehemu utawasili nchini tarehe 11 Oktoba,                  2014 na kuagwa rasmi katika Viwanja vya Karimjee siku ya                  Jumapili tarehe 12 Oktoba, 2014 kabla ya kusafirishwa                  kuelekea Sengerema kwa mazishi.
        Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu                  mahala pema peponi;
        AMINA
        Dkt. Thomas                  Didimu Kashililah
        KATIBU WA CPA KANDA YA                  AFRIKA
                         
