Saturday, September 13, 2014

Balozi Seif akabidhi michango yake wa Wabunge wa Singida


Balozi Seif akabidhi michango yake wa Wabunge wa Singida
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amewapongeza Wabunge na Viongozi wa Mkoa wa Singida kwa kazi kubwa wanazoendelea kuzifanya za kusimamia miradi ya Kiuchumi na ustawi wa Jamii ya wananchi wa Mkoa huo.

Amesema usimamizi huo umeufanya Mkoa huo kuongezeka harakati za maendeleo jambo ambalo wananchi walio wengi wameonyesha muelekeo mkubwa wa kujitegemea kimaisha.

Balozi Seif alisema hayo wakati wa hafla fupi ya kukabidhi michango na kupunguza ahadi alizozitoa wakati wa ziara yake ya hivi karibuni Mkoani Singida aliyoifanya rasmi kama Mlezi wa Mkoa huo Kichama.

Akikabidhi michango hiyo kwa Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki Mh. John Chiligati na Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi Mh.Alhajj Misanga hapo nyumbani kwake Mtaa wa Farahani Mjini Dodoma Balozi Seif alielezea masikitiko yake kwa kuukosa ukarimu wa Wananchi wa Mkoa huo aliouzoea wakati wa ulezi wake.

Balozi Seif katika hafla hiyo fupi alikabidhi mchango wa shilingi Milioni moja na laki Tano kwa ajili ya ununuzi wa mabati ya kuezekea jengo la Mabara ya Skuli ya Sekondari ya Chikuyu iliyopo Wilaya ya Manyoni,shilingi 1,000,000/- za kununulia matofali kwa uendelezaji wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtunduru pamoja na shilingi 1,000,000/- kwa ajili ya Madrasa ya Muzdalifa iliyopo Ilongero.

Balozi Seif pia akakabidhi zawadi za Seti moja moja za Jezi na mipira minne kwa timu za soka na mpira wa pete wa Skuli ya Iyumbu pamoja na skuli ya msingi ya Ilongero.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akimkabidhi Mbunge wa Singida Mashariki Mh. John Chiligati mchango wa shilingi Milioni 1,500,000/- kwa ajili ya ununuzi wa mabati ya kuezekea jengo la Maabara ya skuli ya Sekondari ya Chikuyu Wilaya ya Manyoni kupunguza ahadi aliyoitoa kwa skulio hiyo.
Balozi Seif akimkabidhi Mbunge wa Singida Magharibi Mh. Alhajj Misanga Moja kati ya Seti za jezi na mipira minne kwa timu za soka na mpira wa pete wa Skuli ya Iyumbu pamoja na skuli ya msingi ya Ilongero. Makabidhiano hayo ameyafanya Nyumani kwake Mtaa wa Farahani Mjini Dodoma. Picha na Hassan Issa wa – OMPR – ZNZ.