Monday, December 21, 2015

RAIS AKUTANA NA VIONGOZI MBALIMBALI IKULU



RAIS AKUTANA NA VIONGOZI MBALIMBALI IKULU
maa5

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika AfDB Dkt. Tonia Kandiero Ikulu Jijini Dar es Salaam.

maa6

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuelekeza jambo Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika AfDB Dkt. Tonia Kandiero Ikulu Jijini Dar es Salaam.

maa8

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika AfDB Dkt. Tonia Kandiero Ikulu Jijini Dar es Salaam.

maa9

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na Balozi wa Rwanda hapa nchini Eugene Kayihura aliyefika Ikulu kwa ajili ya mazungumzo.

maa10

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na Balozi wa Rwanda hapa nchini Eugene Kayihura aliyefika Ikulu kwa ajili ya mazungumzo. Picha zote na IKULU


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. amemuhakikishia Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Dkt. Tonia Kandiero kuwa Serikali yake ya Awamu ya Tano itaendelea kushirikiana na benki hiyo katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Dkt. Magufuli amesema hayo leo Tarehe 21 Desemba, 2015 Ikulu Jijini Dar es Salaam, alipokutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi huyo.
Pamoja na kumhakikishia ushirikiano Rais Magufuli ametoa wito kwa benki hiyo kupunguza michakato ya kuelekea katika utekelezaji wa miradi na badala yake ameshauri uwepo utaratibu wa haraka unaowezesha kuanza kwa miradi katika kipindi kifupi baada ya fedha kutolewa.
Kwa upande wake Dkt. Tonia Kandiero pamoja na kumpongeza Rais Magufuli kwa kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika awamu ya tano, amemhakikishia kuwa benki iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika maendeleo kama ambavyo imekuwa ikifanya na kwamba kwa sasa imetenga dola Bilioni mbili nukta tatu kwa ajili ya kufadhili miradi mbalimbali ya maendeleo.
Ameongeza kuwa katika mipango yake ADB imelenga kujielekeza katika utoaji wa mikopo katika sekta ya nishati na usafiri.
Naye Rais Magufuli ameipongeza ADB kwa kuamua kujielekeza katika sekta hizo za nishati na usafiri na pia ameisisitiza kuangalia namna itakavyounga mkono mradi wa ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa yaani standrd gauge.
Katika hatua nyingine Rais wa Jamhuri ya Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Rwanda hapa nchini Mh Uegene Sagore Kayihura Ikulu Jijini Dar es salaam.
Kwa upande wake Rais Magufuli amemuhakikishia Balozi Kayihura kuwa serikali yake ya awamu ya tano itaendelea kushirikiana na Rwanda ili wananchi wa nchi zote mbili waweze kunufaika kimaendeleo.
Katika mazungumzo hayo Balozi Kayihura amewasilisha salamu za pongezi kutoka kwa Rais Paul Kagame wa Rwanda ambaye amempongeza Rais Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa awamu ya tano wa Tanzania.
Balozi Kayihura amesema Rais Kagame amefurahishwa na hatua ambazo Rais Magufuli anazichukua hasa katika usimamizi na utendaji kazi wa bandari na kumhakikishia kuwa Rwanda iko tayari kushirikiana na Tanzania hasa kuitumia bandari ya Dar es salaam ambayo hupitisha asilimia zaidi ya 70 ya mizigo ya Rwanda.
Ameongeza kuwa Rwanda na Tanzania ni nchi marafiki na majirani hivyo kuna kila sababu ya kujenga ushirikiano madhubuti katika sekta ya uchumi.
Rais Magufuli amemuomba Balozi Kayihura kumfikishia Rais Kagame salamu za shukrani kwa kumpongeza kuchaguliwa kuwa rais wa awamu ya tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba amedhamiria kuimarisha zaidi ushirikiano na Rwanda.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
21 Desemba, 2015