Rais wa Jamhuri ya                Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho                Kikwete amemtumia Salamu za Rambirambi Mkuu wa Mkoa wa                Arusha, Mheshimiwa Magesa Mulongo kufuatia ajali ya                barabarani iliyotokea tarehe 30 Oktoba, 2014 katika eneo                la Makumira Wilayani Arumeru katika Mkoa wa Arusha na                kusababisha vifo vya abiria 12 papo hapo na wengine                kujeruhiwa. 
         "Nimeshtushwa na                kusikitishwa sana kutokana na ajali hii mbaya ambayo kwa                ghafla imeondoa uhai wa wenzetu 12 wasio na hatia kutokana                na kukosekana kwa umakini wa binadamu katika uendeshaji wa                vyombo vya moto katika barabara zetu", amesema Rais                Kikwete katika Salamu zake.
        Ameongeza Rais Kikwete:                "Kutokana na ajali hiyo, naomba upokee Salamu zangu za                Rambirambi, na kupitia kwako, Salamu hizi na pole nyingi                ziwafikie wafiwa wote kwa kupotelewa ghafla na wapendwa                wao.  Namuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema azipokee                na kuzilaza Roho za Marehemu wote mahala pema peponi,                Amina".
        Aidha, Rais Kikwete                amewapa pole sana wote walioumia katika ajali hiyo                akimwomba Mwenyezi Mungu awape ahueni ili wapone haraka na                kuweza kurejea katika shughuli za maendeleo yao na yale ya                taifa. "Naomba Mwenyezi Mungu awajalie ahueni ya haraka,                ili muweze kupona haraka na kurejea katika maisha yenu ya                kujitafutia riziki na kuchangia maendeleo ya taifa letu."
        Imetolewa na;
        Kurugenzi ya Mawasiliano                ya Rais,
        Ikulu – Dar es Salaam.
        31 Oktoba,2014
        .bmp)