Wednesday, July 16, 2014

Mbowe Matatani Wilayani Hai..Ana Kesi ya Kujibu Mahakamani


Mbowe Matatani Wilayani Hai..Ana Kesi ya Kujibu Mahakamani
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ameingia matatani baada ya Mahakama ya Wilaya ya Hai kuona ana kesi ya kujibu katika mashtaka ya kumshambulia mwangalizi wa ndani katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Uamuzi huo ulitolewa jana na hakimu mfawidhi wa wilaya hiyo, Denis Mpelembwa mbele ya Mbowe, wakili wake, Issa Rajabu na mwendesha mashtaka, Inspekta Marwa Mwita.

Mpelembwa alisema mashahidi saba wa upande wa mashtaka wameishawishi mahakama kuwa siku hiyo kuna tafrani ambayo ilitokea na ambayo Mbowe

atatakiwa kutoa ufafanuzi wa kuhusika kwake.

Alisema ingawa upande wa utetezi ukiongozwa na wakili Albert Msando na baadaye Rajabu, ulitoa hoja kuwa ushahidi wa Jamhuri uliacha mashimo mengi, yeye anaona Mbowe ana kesi ya kujibu.

"Katika hoja zao (utetezi) wanaona ukiacha ushahidi wa Nassir Yamin, hakuna shahidi mwingine aliyethibitisha kushuhudia Nassir akipigwa," alisema akinukuu hoja za mawakili wa utetezi.

Hakimu aliongeza kusema: "Utetezi pia walitoa hoja kuwa upande wa mashtaka ulishindwa kuwaita akina mama ambao wanaodaiwa kushuhudia, hivyo kuacha mashimo mengi katika ushahidi wao."

Hata hivyo, hakimu alisema katika hoja zao ambazo ziliishawishi mahakama, upande wa mashitaka ulijibu kuwa sheria haiwabani kuleta kila shahidi kujenga msingi wa kesi yao.

"Ni rai yao (mashtaka) kuwa mashahidi wao saba wameweza kuthibitisha shtaka dhidi ya mshtakiwa pasipo kuacha mashaka ama mianya kama utetezi walivyodai," alisema Mpelembwa.

Hakimu Mpelembwa alisema baada ya kupitia hoja za mawakili wa pande zote mbili, anaona upande wa Jamhuri umeweza kuishawishi mahakama kuwa mshtakiwa ana kesi ya kujibu.

Kutokana na uamuzi huo, Hakimu alisema mahakama inampa nafasi Mbowe kujitetea na kesi hiyo imepangwa kutajwa Julai 17, siku upande wa utetezi utakapotoa orodha ya mashahidi wao.

Katika uchaguzi huo mkuu wa 2010, Mbowe aliibuka mshindi kwa kupata kura 28,585 akifuatiwa na Fuya Kimbita (CCM), kura 23,349, Hawa Kihogo (UDP) 258 na Petro Kisimbo (TLP) 135.