Saturday, September 15, 2012

WAZIRI MUHONGO ATANGAZA KIAMA KWA ATAKAYESAINI MIKATABA MIBOVU.



 
Profesa sospeter Muhongo.
Na Datus Boniface.
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo amewaonya maofisa wa Wizara pamoja na wa taasisi zingine zilizopo chini ya Wizara yake kuwa, atakayeliingiza taifa kwenye Mikataba mibovu atafukuzwa kazi na kushtakiwa.
Pia amesema Ofisa anaweza kufukuzwa au kusimamishwa kazi endapo ikibainika kuwa Mkataba aliyousaini una harufu au fununu za rushwa.
Aidha, amewaonya Wakurugenzi wa Bodi ya Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), kuwa hatakuwa tayari kusaini mikataba yoyote, kabla wao kuipitia na kuridhishwa nayo.
Waziri alikuwa akizungumza hayo jijini Dar es Salaam, wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa TPDC.
“Moja ya kazi zenu ni kupitia kila Mkataba na kuona kama una manufaa, lakini pia hakuna Mkataba mpya nitasaini bila Bodi kuupitia” alisema
Alisema uzoefu unaonyesha kuwa pesa nyingi  za serikali hupotea kutokana na mikataba mibovu iliyosainiwa.
Bodi  hiyo mpya  ina wakurugenzi 10 ikiongozwa na Michael Mwinda ambaye ni Mwenyekiti, Robert Kahyoza, na Mwalim Ali Mwalim na wengine.