Na. Ally Mataula –                Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma. 
        Meya wa Halmashauri                Manispaa ya Tabora Mhe. Gulam Hussein Dewji Remtullah                amefikishwa mbele ya Baraza la Maadili kujibu tuhuma                zinazomkabili. 
        Akisoma hati ya                malalamiko mbele ya Mwenyekiti wa Baraza hilo Mhe. Jaji                (Mst.) Hamisi Msumi, Mwanasheria wa Sekretarieti ya                Maadili ya Viongozi wa Umma Bw. Hassan Mayunga alilieleza                Baraza hilo kuwa Mlalamikiwa akiwa Meya wa Halmashauri ya                Manispaa ya Tabora kwa makusudi kabisa alikiuka Maadili ya                Viongozi wa Umma kwa kukiuka kifungu cha 6(a) na (d),                12(1) na 15 (b) vyote vya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa                Umma Na. 13 ya mwaka 1995. 
        Bw. Mayunga                alilifafanulia Baraza kuwa Mhe. Gulam Hussein Dewji                analalamikiwa kwa kujinufaisha binafsi kwa kutumia fedha                kiasi cha shilingi 2,672,000/= mali ya Halmashauri ya                Manispaa ya Tabora kwa ajili ya safari ya nchini Marekani                huku safari hiyo ikiwa imedhaminiwa na kugharamiwa na                Wadhamini waliomualika kutembelea nchini Marekani mnamo                Mwezi Aprili, 2011. Pia, Mhe Gulam Dewji analalamikiwa                kuvunja Sheria ya Maadili makusudi kwa kipindi cha miaka                minne yaani kuanzia mwaka 2010 hadi 2013 kwa kutoa Tamko                la uongo kwa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma                huku akijua kuwa ni kosa kufanya hivyo. 
        Kosa lingine                analolalamikiwa Mhe. Gulam Dewji ni kushindwa kutamka                rasilimali zake ambazo ni pamoja na viwanja Na. 100 kitalu                G, 158 Kitalu G, 637 kitalu D, 99 kitalu F, 206 kitalu C                pamoja na nyumba moja iliyopo kwenye kiwanja Na. 42 kitalu                G vyote vikiwa katika Manispaa ya Tabora. Aidha, Mali                nyingine anazodaiwa kushindwa kuzitamka Mhe. Gulam Dewji                ni pikipiki 422, duka moja, magari namba T 327 ADS Toyota                Hilux, T 842 AWR Toyota Rav4, na T 110 CMW Toyota Rav4. 
         Bw. Mayunga alimaliza                kumsomea hati ya malalamiko Mhe. Gulam Dewji kwa kulieleza                Baraza kuwa kwa kufanya hayo na kushindwa kutekeleza                majukumu yake kwa uadilifu ni ukiukaji wa maadili ya                viongozi wa umma kwa mujibu wa kifungu cha 6(a) na (d),                12(1) na 15(b) vyote ni vya Sheria ya Maadili ya Viongozi                wa Umma. 
         Aidha, Bw. Mayunga                aliliomba Baraza la Maadili lenye mamlaka ya kisheria ya                kufanya uchunguzi wa kina na kumtaka mlalamikiwa kutoa                taarifa bayana kuhusu rasilimali zake na kutoa hati na                kumbukumbu ambazo ziko chini ya udhibiti wake kuhusu                rasilimali hizo kabla ya hatua nyingine kuchukuliwa kwa                mujibu wa sheria. 
        Naye Shahidi wa upande                wa walalamikija Bw. Gerald Mwaitebele ambaye ni Mtumishi                wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya                Magharibi - Tabora alilieleza Baraza la Maadili kuwa Ofisi                ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma – Kanda ya                Magharibi Tabora walipata tuhuma saba za ukiukaji wa                Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma dhidi ya Mlalamikiwa                kupitia vyombo vya habari. 
        Bw. Mwaitebele                aliendelea kulieleza Baraza hilo kuwa baada ya kufanya                uchunguzi wa awali walifanikiwa kupata ushahidi kwa                malalamiko matatu na mengine hawakuweza kupata ushahidi na                hivyo kuamua kuyaacha. 
         Kwa mujibu wa Bw.                Mwaitebele tuhuma ambazo waliweza kupata uthibitisho baada                ya uchunguzi wa awali ni pamoja na kutumia madaraka vibaya                kwa kujinufaisha fedha za Halmashauri ya Manispaa ya                Tabora, kutumia vibaya madaraka kwa kujitwalia mali ambazo                ni viwanja na kutoa tamko la uongo kwa kushindwa kutaja                mali zake yeye binafsi, mke pamoja na watoto wake. 
        Hata hivyo Mlalamikiwa                Mhe. Gulam Hussein Dewji alikana malalamiko yote dhidi                yake na Mwenyekiti wa Baraza la Maadili Mhe. Jaji (Mst.)                Hamisi Msumi aliahirisha kusikiliza shauri hilo hadi                tarehe nyingine itakayotangazwa hapo baadae. 
        Baraza la Maadili ni                chombo cha kisheria chini ya fungu la 26 la Sheria ya                Maadili ya Viongozi wa Umma lenye mamlaka ya kufanya                uchunguzi wa kina kuhusu malalamiko yanayohusu ukukaji wa                Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma dhidi ya kiongozi                yeyote. 
         Kwa mujibu wa fungu la                26 (8) linasema kuwa katika taarifa yake, Baraza linaweza                kutoa mapendekezo kuhusu hatua za kiutawala, mashitaka ya                jinai au hatua nyingine zozote za kuchukuliwa dhidi ya                kiongozi husika kwa kadri litakavyoona inafaa. 
                 Mstahiki                  Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Mhe. Gulam                  Hussein Dewji (aliyeshika chupa ya maji) akizungumza na                  Waandishi wa Habari mara baada ya kutoka kuhojiwa na                  Baraza la Maadili juu ya tuhuma zinazomkabili kuhusu                  ukiukaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma katika                  Ukumbi wa Karimjee, Jijini Dar es Salaam.
        Shahidi upande wa                    Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bw. Gerald                    Mwaitebele kushoto akizungumza na Mwanasheria wa                    Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Bw.                    Filotheus Manula mara baada ya kutoa ushahidi wake                    kuhusu tuhuma za ukiukaji wa Sheria ya Maadili                    zinazomkabili Meya wa Manispaa ya Tabora  Mhe. Gulam                    Dewji mbele ya Baraza la Maadili katika Ukumbi wa                    Karimjee, Jijini Dar es Salaam.
        .jpg)
.jpg)
 
