Friday, October 28, 2011

Neno La Leo: Mchwa Anapokaribia Kufa Huota Mbawa

Ndugu zangu,

Kuna tuliomsoma mwanafasihi Shaaban Robert.  Kuna mahali kwenye kitabu chake ' Nchi Ya Kusadikika' Shabaan Robert  anamwelezea mchwa anayekaribia kufa.

Kwamba huota mbawa. Hukiacha kichuguu . Yumkini ataruka juu sana. Atakwenda mbali.  Lakini, huko angani hufika mahali, mbawa hupukutika. Mchwa ataanguka chini. Mbali na kichuguu.

Hapo, mchwa hukabiriwa na  hatari kubwa.  Hawezi kuruka tena, na yu mbali na kichuguu.  Na kichuguu ni taasisi. Hivyo, mchwa  anaweza kuliwa na kinyonga, au hata chura. Na akinusurika na wawili hao, aweza kukanyagwa na unyayo wa mwanadamu, au hata tairi la baiskeli. Mchwa atakufa.

Naam, mengine tuyafanyayo hupelekea maanguko yetu. Hata kama mwanzoni huonekana kutupaisha juu angani.

" Nafikiri, ndio maana naishi"- Anasema mwanafalsafa Rene Descartes. 

Na maarifa ya Sayansi  yanatusaidia kuyabaini mahusiano kati ya dunia tunayoishi na mazingira yanayotuzunguka. Hiyo ni falsafa ya kivitendo. Ndio iliyo bora kuliko ile dhanifu- Speculative.

Iweje basi tumekuwa ni  watu wa  kuishi kwa  dhania na hata kusambaza uvumi?

Ngoja nijiandae kwa safari yangu ya Iringa kesho alfajiri.
Usiku mwema.
Maggid
Msamvu, Morogoro.
http://mjengwa.blogspot.com