Sunday, November 29, 2015

BOMOBOMOA SALASALA ILI KUPISHA UJENZI WA BOMBA LA MAJI -RUVU CHINI



BOMOBOMOA SALASALA ILI KUPISHA UJENZI WA BOMBA LA MAJI -RUVU CHINI
  Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Zoezi la kubomoa nyumba na majengo yaliyoingia ndani ya ya hifadhi ya miundombinu ya bomba la maji kutoka Ruvu Chini limeendelea mwishoni mwa wiki ili kuhakikiha kunakuwepo usalama wa bomba hilo na kuwapatia wakazi wa jiji la Dar es salaam na maeneo ya mkoa wa Pwani uhakika wa maji ifikapo Februari, 2016.  
Bomo bomoa hiyo ya mwishoni mwa wiki ilihusisha maeneo ya Salasala ambapo baadhi ya nyumba, karakana na uzio vyote viljengwa ndani ya hifadhi ya miundombinu hiyo ya maji.
Akizungumzia ubomoaji huo, Mkurugenzi wa Usimamizi na Ufundi wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA), Romanus Mwang'ingo alisema kuwa ni wajibu wa wakazi wa maeneo hayo kuvunja sehemu za makazi yao yaliyoingia ndani ya hifadhi ya mradi kwa hiyari ama nyumba hizo kuvunjwa baada ya kukaidi agizo la kubomoa ili kupisha ujenzi wa bomba la maji kutoka Ruvu Chini hadi jijini Dar es salaam.
"Umbali sahihi unaopaswa wakazi hao kujenga makazi yao kutoka lilipo bomba la maji ni mita 15 kila upande ambapo hatua hiyo inapelekea kuwa jumla ya mita 30 ya umbali unaotakiwa ili kuhakikisha kunakuwepo na usalama na kuruhusu matengenezo mengine tofauti na hali ya awali ambayo huwezi hata kufanya kazi maana bomba limepita ndani ya uzio na makazi ya watu ambayo ni hatari kwa usalama wa maisha yao na mali zao" alisema Mwang'ingo.
Vile vile Mwang'ingo alizitaja changamoto zilizochangia kuchelewesha kukamilika kwa mradi huo kwa wakati ni kuwepo kwa kesi zilizofunguliwa na wananchi kuzuia ufanisi wa kazi hiyo ambapo kulikuwa na kesi 17 katika mahakama mbalimbali katika maeneo hayo ikiwemo mahakama ya ardhi. 

Kwa mujibu wa Mwang'ingo hadi sasa DAWASA imeshinda kesi 13 na kupewa haki ya kutumia njia hiyo kukamilisha upanuzi wa mradi na zimebaki kesi nne ambazo bado zipo mahamani na zimefikia hatua mbalimbali kulingana na taratibu za kimahakama.
Kwa upande wake mkazi wa Salasala Mhandisi Josephat Nakapange ambaye sehemu ya nyumba yake pamoja na uzio vipo ndani ya hifadhi hiyo ya bomba la maji kutoka Ruvu Chini hadi Dar es salaam alisema kuwa yeye hana tatizo wala ugomvi na mradi huo, wamepokea maelekezo na wanayafanyia kazi.
"Hivi sasa ninavyoongea mafundi wapo kwenye eneo langu wanaendelea na zoezi la kutoa mabati na baadaye kuvunja kuta zilizo ndani ya umbali unaotakiwa kuachwa wazi kwa ajili ya mradi wa bomba la maji" alisema Josephat.
Aidha, Josephat aliongeza kuwa ni vema ziwekwe alama katika maeneo yote yanayotakiwa kuachwa wazi ambayo yapo ndani ya hifadhi ya mradi ili kuepusha usumbufu na gharama zisizo za lazima kwa wakazi ulipopita mradi huo.
Maeneo yaliyohusishwa na ubomoaji huo mwishoni mwa wiki ni pamoja na Bunju, Bondeni, Boko, Tegeta, Mbezi Intacheki, na Mbezi Tangibovu ili kuruhusu kukamilisha ujenzi wa bomba hilo la maji kutoka Ruvu Chini ha jijini Dar es salaam.
Tingatinga likishushwa tayari kwa kazi ya bomobomoa eneo la Salasala jijii Dar es salaam ili kupisha ujenzi wa bomba la maji kutoka Ruvu Chini hadi jijini Dar es salaam.
 Kazi ya kubomoa baadhi ya nyumba ikiendelea mwishoni mwa wiki eneo la Salasala jijii Dar es salaam ili kupisha ujenzi wa bomba la maji kutoka Ruvu Chini.
  Tingatinga likisukuma na kung'oa miti na jengo eneo Salasala iliyo  ndani ya hifadhi ya bomba la maji kutoka Ruvu Chini hadi jijini Dar es salaam jijii Dar es salaam.
  likisukuma na kung'oa mnazi eneo Salasala ambao upo ndani ya hifadhi ya bomba la maji kutoka Ruvu Chini hadi jijini Dar es salaam jijii Dar es salaam.
  Tingatinga likisukuma na kung'oa mnazi eneo Salasala ambao upo ndani ya hifadhi ya bomba la maji kutoka Ruvu Chini hadi jijini Dar es salaam jijii Dar es salaam.

Mafundi wakiendelea kubomoa nyumba iliyopo eneo la Salasala kwa hiyari ya mmiliki wa nyumba hiyo ili kupisha ujenzi wa bomba la maji kutoka Ruvu Chini. (Picha na Eleuteri Mangi-MAELEZO)