Sunday, January 25, 2015

Escrow yapangua mawaziri 13... SLAA ASEMA HAKUNA JIPYA, ni walaji wale wale..



Escrow yapangua mawaziri 13... SLAA ASEMA HAKUNA JIPYA, ni walaji wale wale..


Hatimaye Rais Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko 13 kwenye Baraza la Mawaziri yaliyohusisha mawaziri nane, manaibu watano, wakiwamo wapya wawili, ikiwa ni siku mbili kabla ya kuanza kwa Bunge, na ndani ya saa 48.

Rais pia aliwaapisha mawaziri wote 13 akiwamo waziri mpya wa Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe ambaye alisababisha hafla hiyo kuchelewa kwa kuwa alikuwa akitokea Davos, Uswisi.

Mabadiliko hayo, yanayoweza kuwa ya mwisho kwa Rais Kikwete, yamefanyika ikiwa imesalia miezi sita kabla ya kuvunjwa kwa Bunge kupisha Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba.

Rais amelazimika kufanya mabadiliko hayo baada ya mawaziri wawili, Profesa Anna Tibaijuka na Profesa Sospeter Muhongo, kuondoka kutokana na kuhusishwa na kashfa ya uchotwaji fedha kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, ambayo pia imesababisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliackim Maswi kusimamishwa kazi, huku waziri wa zamani wa wizara hiyo, William Ngeleja akivuliwa uenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria.

Kwa mujibu wa mabadiliko hayo, Kikwete amewaondoa mawaziri wawili wazoefu kutoka Ofisi ya Rais, Steven wasira na Ofisi ya Waziri Mkuu, William Lukuvi, kuwapangia wizara nyingine, huku akimhamishia Dk Mary Nagu kwenye Ofisi ya Rais na Jenister Mhagama (Waziri Mkuu).

Akitangaza mabadiliko hayo jana, Katibu Mkuu Kiongozi Ombeni Sefue alisema mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene, ambaye alikuwa naibu wa wizara ya Nishati na Madini kuanzia mwaka 2012 hadi 2014 na ambaye hadi jana alikuwa naibu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ameteuliwa kumrithi Profesa Muhongo kwenye wizara hiyo tata ya Nishati na Madini.

Simbachawene anakuwa waziri wa nne kushika wizara hiyo tangu Serikali ya Awamu ya Nne iingie madarakani na anaingia wakati Steven Masele, aliyekuwa naibu Waziri wa Nishati na Madini, akiwa amehamishiwa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano). Nafasi ya Masele imechukuliwa na mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage ambaye ameteuliwa kwa mara ya kwanza.

Sefue alisema mbunge wa Ismani, William Lukuvi, ambaye tangu mwaka 2010 amekuwa Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Utaratibu na Bunge), ameteuliwa kuziba nafasi ya Profesa Tibaijuka ya uwaziri wa Kazi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Sura nyingine ngeni kwenye baraza hilo, kwa mujibu wa Sefue, ni ya mbunge wa Same, Anne Kilango Malecela, mmoja wa wazungumzaji wakubwa bungeni, ambaye ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu.

Alisema aliyekuwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama amepanda kuwa Waziri wa Nchi, Sera, Uratibu na Bunge, nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Lukuvi.

Nagu amehamia Uhusiano na Uratibu (Uwekezaji na Uwezeshaji) na Dk Harrison Mwakyembe anayehamia Afrika Mashariki (Uchukuzi).

Wengine ni mwanasiasa mkongwe, Steven Wasira aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Kilimo akitokea Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, wakati Samuel Sitta anakwenda Uchukuzi akitokea Wizara ya Afrika Mashariki.

Manaibu waziri wengine waliohamishwa ni Angella Kairuki, ambaye anakwenda Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi akitokea Katiba na Sheria.

Ummy Mwalimu anakuwa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria akitokea Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira).

Mabadiliko hayo yamekuja ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio manane ya Bunge, kutaka uteuzi wa Profesa Muhongo na Profesa Tibaijuka kutokana na kuhusishwa na kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow.

Bunge liliagiza mamlaka ya uteuzi kutengua nyadhifa hizo pamoja na wenyeviti wa Kamati za Bunge, Nishati na Madini iliyokuwa chini ya Victor Mwambalaswa.

Wengine waliotakiwa kuvuliwa nyadhifa za Kamati kutokana na kashfa hiyo ni Andrew Chenge (Bajeti) na Kamati ya Sheria na Katiba iliyokuwa chini ya William Ngeleja.

Akizungumzia uteuzi huo, Kilango alisema: "Ninayajua matatizo ya walimu wenzangu na kwa kushirikiana na wenzangu tutaweza kuyatatua, kikubwa ni kushirikiana."

Alisema kuwa kwa kushirikiana na Waziri wa Wizara hiyo watakuja na mipango na mikakati itakayolenga kuboresha sekta ya elimu.

Kwa upande wake, Lukuvi alisema kuwa anafahamu changamoto zinazoikabili wizara hiyo na atashirikiana na wananchi ili kuzitafutia ufumbuzi.

"Ninachoomba ni ushirikiano kutoka kwa wananchi kwa kuwa ni imani yangu kuwa tukiunganisha nguvu zetu kwa pamoja kazi itafanyika vizuri"alisema Lukuvi

Naye Waziri wa Nishati na Madini George Simbachawene alisema anatambua fika kuwa uchumi wa nchi yeyote unategemea nishati hivyo atahakikisha sekta hiyo inawaletea manufaa watanzania wote.

Simbachawene alisifu kazi ya Profesa Muhongo ana akasema atahakikisha anaikamilisha kwa kufikisha umeme kote vijijini.

Dk Slaa alonga

Akizungumzia mabadiliko hayo, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema: "Hakuna jipya katika hayo mabadiliko, kwani tatizo lililopo ni mfumo na si viongozi, Watanzania wasitegemee lolote kutoka kwao.

"Kitendo hiki cha watu wanafanya makosa halafu wanaachiwa wanajiuzulu na kubaki na sifa zao.

Kama taifa hatuwezi kusonga mbele. Tunahitaji kuwashughulikia wanaorudisha nyuma maendeleo ya nchi."

Katibu huyo aliongeza kusema: "Wahalifu bado wanapata fursa ya kukaa na kujadiliana na rais, hii haikubaliki. Washabainika wamefanya makosa kwa nini wasiwajibishwe mapema?"

TBC yawa kero

Shirika la Habari Tanzania (TBC) jana liliwakera Watanzania waliokuwa wakifuatilia matangazo ya moja kwa moja ya mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri.

Mabadiliko hayo yalikuwa yakitangazwa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue kutoka Ikulu jijini Dar es Salaam ambapo yalihusisha mawaziri na manaibu mawaziri.

Matangazo hayo yalikuwa yakikatika mara kwa mara na wakati mwingine yakionyesha picha bila sauti jambo lililokuwa kero kwa watazamaji.

Hata hivyo, mkurugenzi mtendaji wa TBC, Clement Mshana alipotafutwa kuzungumzia matatizo yaliyojitokeza, alisema kwa kifupi "mimi sijui na nipo mkoani ninaendelea kufuatilia matangazo ya mabadiliko hayo" na kukata simu.

Katika hatua ya uapishwaji wa mawaziri na manaibu mawaziri hao ulioanza Saa 12.14 jana jioni muda mfupi baada ya kumalizwa kutangazwa matangazo yaliendelea vizuri.

Hali hiyo si ya kwanza kutokea kwani katika mijadala kadhaa ya mikutano ya Bunge matangazo yamekuwa yakikatika jambo lililokuwa likilalamikiwa na baadhi ya wabunge na wananchi kwa kukoseshwa fursa ya kutazama muhimili huo wa ukiendelea na shughuli Zake.